Maambukizi ya Ukimwi yapungua Lindi

Muktasari:

Mratibu wa Ukimwi wa Mkoa wa Lindi, Dk Enock Chilumba amesema maambukizi ya Ukimwi katika Mkoa wa Lindi yamepungua kutoka asilimia 3.9 mwaka 2008 hadi asilimia 0.3 mwaka 2017.

Lindi. Mambukizi mapya ya ugonjwa wa Ukimwi katika Mkoa wa Lindi yamepungua kutoka asilimia 3.9 mwaka 2008 hadi asilimia 0.3 mwaka 2017.

 Takwimu hizo zimetolewa leo Septemba 26 na Mratibu wa Ukimwi wa mkoa huo, Dk Enock Chilumba kwenye mafunzo ya viongozi wa dini kuhusu ugonjwa huo kupitia mradi wa Afya Yangu unaofadhiliwa na Shirika la Missada la Marekani Usaid wenye lengo la kupunguza maambukizi mapya. 

Amesema kuwa mwaka 2008 mkoa huo ulikuwa juu kwa maambukizi kwa asilimia 3.8 wakati mwaka 2012 ulikuwa na asilimia 2.9 na utafiti wa mwaka 2017  maambukizi yamepungua na kufikia asilimia 0.3

Dk Chilumba amesema maambukizi hayo yamepungua kutokana na jitihada zilizofanywa na serikali kwa kushirikiana na wadau katika utoaji wa elimu na namna ya kujikinga na ugonjwa huyo.

“Awali maambukizi yalikuwa makubwa kwa sababu elimu na uelewa wa jamii ulikuwa mdogo, lakini mafanikio makubwa yaliyopatikana sasa yametokana na upimaji wa Ukimwi kwa hiari katika vituo vya kutolea huduma, kwenye maeneo ya mikusanyiko, ufuatiliaji na usimamizi wa karibu kwa watu wanaotumia dawa zakufubaza,” amesema Dk Chilumba.    

Ameongeza kuwa Mkoa wa Lindi una vituo 130 vya kutolea huduma kwa wagonjwa wa ukimwi ambapo jumla ya watu 26,743 wanatumia dawa za kufubaza virusi.   

Kwa upande wake kiongozi wa dini, Sheikh Mohamedi Mshangani amesema mafunzo hayo yataongeza uelewa kwa viongozi wa dini na kufikisha ujumbe kwa waumini wao kwa usahihi.

“Ni wajibu wetu kama viongozi wadini kutoa elimu ya maambukizi ya ukimwi kwa waumini wetu ili kusaidia serikali kufikia malengo ya kupambana na ugonjwa huyo,” amesema Sheikh Mshangani.

Amesema ili kupunguza janga hilo kwenye jamii ni jukumu la viongozi wa dini kukemea maovu na kuwataka waumini kuongozwa na maadili kupitia maandiko matakatifu.