Madiwani watakiwa kuachana na migogoro

Madiwani watakiwa kuachana na migogoro

Muktasari:

  • Madiwani 29 wa Halmashauri ya Buchosa Wilayani Sengerema Mkoa wa Mwanza wamepata mafunzo ya kanuni za kudumu za uendeshaji wa Halmashauri yao.

Sengerema. Madiwani wa Halmashauri ya Buchosa Wilayani Sengerema Mkoa wa Mwanza wametakiwa kuachana na migogoro inayodidimiza maendeleo, badala yake wasimamie masuala yenye masilahi ya umma.

Kauli hiyo imetokewa leo Oktoba 12 na Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Senyi Ngaga alkiyewakilishwa na Katibu tawala wa Wilaya ya Sengerema, Allen Augustine kwenye mafunzo elekezi juu ya uendeshaji wa Halmashauri kwa madiwani wa Buchosa.

Amesema watumie mafunzo haya kuwasidia kusimamia masilahi ya umma na kuachana na migogoro ambayo inarudisha nyuma maendeleo ya wananchi.

"Tunapaswa kuwa wazalendo na kusimamia masilahi ya umma na ili Halmashauri zetu zisinge mbele mafunzo haya yatakiwa chachu ya maendeleo kwenye maeneo yenu," amesema Ngaga.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Buchosa, Paul Malala amesema wameona vema kutoa mafunzo hayo kwa madiwani lengo nikuwajengea uwezo kutambua majukumu yao na kuondoa migogoro isiyo ya lazima.


Naye mwezeshaji toka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Oscar Tandula amesema katika mafunzo hayo madiwani wanafundishwa juu ya kaununi za kudumu za uendeshaji wa Halmashauri.

Pia amesema wanafundishwa kuhusu sheria ya maadili ya viongozi wa umma namba 13 ya 1995, sheria na kanuni za maadili ya viongozi wa umma, udhibiti wa migongano wa masilahi za mwaka 2020.

Sambamba na mahusiano ya kisheria Kati ya Serikali kuu na serikali za mitaa, wajibu, majukumu, haki na stahiki za madiwani pamoja na wajibu wa Diwani katika kuibua, kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo.

"Tunawapitisha kwenye maada hizi wazielewe, kwani zitasaidia kujua majumu yako ya kusimamia Halmashauri yao na kuepuka migogoro isiyo na tija kwa masilahi ya Wananchi," amesema Tandula.

Diwani wa viti maalumu kutoka tarafa ya Kahunda, Mwamini Gandama amesema mafunzo hayo waliyopata yatawasaidia kusimamia vema majukumu yao hasa katika kutekeleza miradi ya maendeleo.