Mahakama yatupa pingamizi kesi ya Sabaya

Mahakama yatupa pingamizi kesi ya Sabaya

Muktasari:

  • Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, imetupilia mbali pingamizi lililowasilishwa na upande wa utetezi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake sita.

Arusha. Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, imetupilia mbali pingamizi lililowasilishwa na upande wa utetezi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake sita.

Sabaya na wenzake sita leo Alhamisi Septemba 30, 2021 waliwasilisha pingamizi dogo la kisheria, wakipinga mahakama hiyo isipokee daftari la kumbukumbu ya magari yanayoingia na kutoka katika gereji ya mfanyabiashara, Francis Mrosso

Hakimu Mkazi Patrisia Kisinda ametoa uamuzi huo mdogo akisema kwa sababu shahidi huyo namba tatu ana ufahamu wa nyaraka anazotaka kuziwasilisha mahakamani hapo na nyaraka hizo zipo kwenye umiliki wake, zinapokelewa mahakamani hapo kama vielelezo.

Leo shahidi wa tatu wa Jamhuri katika kesi hiyo, Adanbest Marandu, ambaye ni mlinzi katika gereji  hiyo alianza kutoa ushahidi wake akiongozwa na  wakili wa Serikali mwandamizi Tarsila Gervas.

Shahidi huyo aliiomba mahakama ipokee daftari hilo kama kielelezo katika shauri hilo,ombi ambalo lilipingwa na mawakili wa utetezi, Mosses Mahuna, Fridolin Gwemelo na Edmund Ngemela.

Akiwasilisha hoja za  pingamizi hilo, wakili Mahuna aliieleza mahakama kuwa kabla ya kitabu kutolewa, wamekiona kikitoka kwenye mikoba ya wakili Tarsila na kuwa hawaelewi yeye binafsi amekipata wapi na kumtaka shahidi akitoe mahakamani hapo.