Majaliwa awataka MaDC kuwaeleza wakulima kilimo kitakavyowanufaisha

Majaliwa awataka MaDC kuwaeleza wakulima kilimo kitakavyowanufaisha

Muktasari:

  • Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka wakuu wa wilaya wanapokwenda kuhamasisha kilimo kwa wananchi wawape hesabu namna watakavyonufaika.

Singida. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka wakuu wa wilaya wanapokwenda kuhamasisha kilimo kwa wananchi wawape hesabu namna watakavyonufaika.

Majaliwa amesema hayo leo Jumapili Juni 13, 2021 kwenye mkutano wa kampeni ya kitaifa ya alizeti unaofanyika mkoani Singida.

Amesema kumhamasisha mkulima alime zao au mazao mengine kunahitaji umueleze namna gharama za kilimo kuanzia mwanzo kwamba atatumia kiasi gani na atanufaika vipi.

Majaliwa amewataja wakuu wa wilaya kuacha kutoa maelezo ya jumla katika kilimo kwa wakulima na badala yake wawaeleze gharama zitakazotumika kwenye kilimo na faida atakayopata.

Pia, amewataka wenye mabenki kutoa mikopo kwa wakulima ili kuwawezesha kupata mitaji na kulima kilimo chenye tija.

Pia, amewataka wakuu wa wilaya kuwa makini na viwanda vinavyokamua mbegu za alizeti kwa ajili ya mafuta kwa kuwa kuna maeneo wakulima wanaibiwa.

Ametoa mfano wa mwenye kiwanda mmoja aliyetanua mashine zake na ikawa inakamua mafuta kidogo kwa lengo la kuwaibia wakulima.