Majirani wasimulia mtoto aliyeua baba yake na dada

Kamanda wa polisi Mkoani Mwanza, Jumanne Muliro

Mwanza. Majirani wa familia ya mchungaji wa kanisa la Hakuna kama Yesu, Benedicto Ndyanabo aliyeuawa kwa kuchomwa kisu na mtoto wake wilayani Ilemela jijini Mwanza, wamesema kijana huyo pia alitaka kuwachoma na wao kabla ya kudhibitiwa.

Katika tukio hilo, Richmond Kalenga (32), pia alimuua Dada yake Renata Benedict kwa kumchoma visu sehemu mbalimbali za mwili wake.

Anitha Jerome jirani wa familia hiyo, alisema kwamba walikuwa wakijiandaa kwenda kanisani lakini wakasikia vilio vya kuomba msaada.

“Renata alikuwa akimpa mtoto chai kwenda kanisani, kidogo yule kijana akatoka nje akiwa na kitambaa chekundu akamchoma kisu dada yake kumbe ametoka ndani akiwa ameshamchoma tayari baba yake”

Kamanda wa polisi wa Mkoa huo, Jumanne Muliro alisema kwamba tukio hilo lilitokea Januari 15 saa tisa alasiri.

Hata hivyo, kamanda Muliro alisema baada ya kijana huyo kutenda tukio hilo, alishambuliwa na wananchi waliofika nyumbani hapo kutoa msaada ambapo na yeye alifariki dunia akiwa njiani akikimbizwa katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo.