Mambo 10 yaibuka operesheni za Chadema nchi nzima

Mambo 10 yaibuka operesheni za Chadema nchi nzima

Muktasari:

  • Wakati viongozi waadnamini wa Chadema wakifisha siku ya saba katika ziara zao mikoani, mambo 10 yamejitokeza katika vikao hivyo vya ndani.

Dar es Salaam. Wakati viongozi waadnamini wa Chadema wakifisha siku ya saba katika ziara zao mikoani, mambo 10 yamejitokeza katika vikao hivyo vya ndani.

Mambo hayo ni kuipeleka Chadema kidijitali, matumizi ya kadi za kieletroniki, kudai Katiba Mpya, kujipanga na uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka 2024 na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, naa kuangalia uwezekano wa kutoshiriki uchaguzi mazingira yasipokuwa rafiki.

Mengine ni Chadema kujiendesha kwa mapato yake, kuanzisha chuo cha mafunzo ya itikadi, ujenzi wa ofisi za chama hicho, kutoshiriki pamoja na tume huru ya uchaguzi.

Ziara ya viongozi hao wakiongozwa na mwenyekiti wao Taifa, Freeman Mbowe ilianza Mei 25 mwaka huu mkoani Arusha walipokutana na kuzungumza na viongozi wa kamati ya utendaji wanaotoka mikoa ya Kilimanjaro, Manyara, Tanga na Arusha.

Kwa sasa viongozi hao wapo mkoani Shinyanga wanakozungumza na wajumbe wa kanda ya Serengeti yenye mikoa ya Mara na Simiyu katika ziara iliyopewa jina la ‘operesheni haki’ iliyopangwa kufanyika kwenye kanda 10 za chama hicho, Bara na visiwami.

 Ziara ya viongozi hao leo (Jumatatu) inahitimishwa kanda ya Serengeti kabla ya kesho kuanza kanda ya Victoria. Akiwa Jjjini Arusha, Mbowe aliwaeleza viongozi wa kanda ya Kaskazini kuwa Chadema imejipanga kuendesha shughuli zake kidijitali kuanzia uandikishaji na usajili wa wanachama.

 Alisema kadi walizonazo sasa zitakuwa kumbumbuku kwao badala yake watatakiwa kuwa na kadi mpya za kisasa zilizobuniwa kitaalamu na kugawanywa kwenye madaraja matano kulingana na uwezo wa mwanachama husika.

“Kadi ya kiwango cha chini italipiwa Sh25,000 kwa mwaka inaitwa ‘bluu kadi’ iliyonakshiwa kitaalamu pasipo kuingiza maji. Nyingine ni silver inayofanana na kadi ya benki itakayolipiwa Sh200,000. Kuna kadi ya dhahabu yenye thamani ya Sh50,000. Kuna kadi ya Sh100,000 inayoitwa almasi.

Kila mwanachama atalipa kulingana na uwezo wake na wote watakuwa na haki ya kugombea na kupiga kura,” alisema Mbowe. Mwenyekiti huyo amewataka wanachama na viongozi wa Chadema kujiweka sawa kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka 2024 na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 na kuwakumbusha kutokata tamaa kwani muda uliobakini mfupi sana.

Hata hivyo, alisema Chadema hakishiriki uchaguzi kama hakutapatikana tume huru itakayosimamia mchakato huo. Vilevile, alisema Chadema wana mpango wa kuanzisha chuo cha itikadi kitakachoitwa Edwin Mtei Leadership Academy kitakachojenga misingi ya imani kwa wanachama wake kukabili wimbi la kukihama.

 Jambo jingine alilosisitizia katika ziara hizo ni Chadema kutekeleza mpango wa kujiendesha kwa mapato kikitumia taarifa za kijdijitali za wanachama wake.

Alisema kupitia mfumo huo wataandikisha upya wanachama wao na kuwahamasisha kuchangia ada zao za uanachama. Mapato yatakayopatikana, alisema yatatumika kujenga ofisi za makao makuu ya majimbo na ofisi za kitaifa hivyo kuwahimiza viongozi wa wilaya hadi kanda.

Naibu katibu mkuu wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu alisema ziara hiyo imejikita kuunganisha wanachama wao na kuweka mikakati bora ya kujiandaa na uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025. “Tunahimiza suala la tume huru ya uchaguzi, sio kwamba tunataka jambo hilo kwa faida ya Chadema bali linahitaji ili kuweke misingi mizuri na imara ya uchaguzi. Tunataka tuondokane na changamoto zilizojitokeza kwenye chaguzi zilizopita,” alisema Mwalimu.

Wakati Mwalimu akieleza hayo, kaimu mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Sharifa Suleiman alisema wao wamejikita kupaza sauti kwa wanawake kupitia vikao hivyo kuhusu tume huru ya uchaguzi.

Kwa upande wake, mwenyekiti wa Baraza la Vijana (Bavicha), John Pambalu alisema ajenda yao kubwa ni kuwaelemisha vijana umuhimu wa Katiba Mpya.