Mke wa Sabaya atoa ushahidi

Muktasari:

  • Mke wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya, Jesca Thomas (28) ameieleza Mahakama namna walivyokamatwa na mume wake na askari waliokuwa na silaha jijini Dar es Salaam.

Arusha. Mke wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya, Jesca Thomas (28) ameieleza Mahakama namna walivyokamatwa na mume wake na askari waliokuwa na silaha jijini Dar es Salaam.

Jesca ambaye ni shahidi wa pili wa utetezi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili Sabaya na wenzake sita ameieleza Mahakama kuwa alikamatwa na mume wake Mei 27 mwaka jana jijini Dar es Salaam ambapo alidai kabla ya kukamatwa walipekuliwa na askari hao waliokuwa wamevalia kiraia huku wakiwa na silaha.

Leo Januari 17, 2022 akiongozwa na Wakili Mosses Mahuna anayemtetea Sabaya, Jesca alijitambulisha mahakamani hapo kuwa ni mke wa mshitakiwa huyo na walifunga ndoa mwaka 2018.

"Tukiwa chumbani walikuja watu usiku, walikuwa wanagonga kwa nguvu sana na hawakusubiri kufunguliwa walitumia njia zao wakaingia ndani ilikuwa ni saa 10 jioni. Walivyoingia Lengai akauliza ni nini na ni nani nyie, wakajibu wakasema ni askari wakatuamuru tukae sehemu moja,"

"Wengine wakawa wanapekua kabati mabegi wakatoa na godoro wakapekua kila mahali, vurugu kila kitu kikavurumushwa kule ndani,walivyomaliza wakasema tunaondona na nyie tunaenda Takukuru,na hawakutufahamisha chochote kabla ya kutupekua," amedai

Shahidi huyo amedai mahakamani hapo kuwa walikamatwa wao wawili na baada ya kutoka makao makuu ya Takukuru, Upanga walisafirishwa Juni 3 usiku na kufikishwa Arusha ambapo pamoja na vitu vingine walikabidhi gari aina ya Land Cruiser V8, lenye namba za usajili T 222 BDY ambayo walikutwa nayo, pesa pamoja na simu.

Amedai gari hilo Sabaya alinunua Oktoba 2020 kutoka kampuni ya Oil Com na ambaye alisimamia mauziano hayo alimtaja kwa jina la Said.

Kuhusu namba ya simu 0758 707171 inayodaiwa kuwa ya Sabaya, Jesca ameieleza mahakama kuwa namba hiyo imesajiliwa kwa jina la mume wake na wamekuwa wakiitumia wote ambapo yeye anaitumia kwa ajili ya kufanya biashara.

Akihojiwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Ofmed Mtenga shahidi huyo alidai kuwa wana magari mawili ambayo yote ni Land Cruiser VX V8 yote yanashikiliwa Takukuru


Sehemu ya mahojiano hayo yalikuwa kama ifuatavyo;



Wakili: Nikumbushe majina yako


Shahidi: Jesca Thomas Nassari


Wakili: Wewe na Lengai Sabaya hamjawahi kufunga ndoa

Shahidi:Tumefunga ndoa


Wakili: Mlifunga ndoa lini?


Shahidi: Sabato Central Church mwaka 2018



Wakili: Cheti cha ndoa cha hilo kanisa unacho?


Shahidi:ndiyo 



Wakili:Kipo nyumbani mna mpango gani?


Shahidi:Kikihitajika nitakileta



Wakili:Leo ulijua unatoa ushahidi mbona hukukileta?


Shahidui:Sikuwa nakuja kuthibitisha ndoa ndiyo mana sikukileta



Wakili:Umekuja kufanya nini?


Shahidi:Kutoa ushahidi wa kesi inayoendelea mahakamani lakini si ya ndoa 



Wakili:Tutajie wasimamizi wa ndoa yenu


Shahidi:Ni Elibariki Nnko na Ruth Urassa



Wakili:Wako hapa Arusha


Shahidi:Wanakaa Dar Es Salaam





Wakili:Umesema  unafanya biashara gani?


Shahidi:Nauza na kununua maharage na mahindi



Wakili:Unauza kibaba debe au gunia?


Shahidi:Inategemea mteja anahitaji kiasi gani 



Wakili:Una warehouse ya kuhifadhi mazao ghala liko wapi?



Shahidi :Kisongo na lingine liko Tengeru



Wakili:Umekodi kwa nani?


Shahidi:mzee Metili



Wakili:Kiasi kikubwa cha mahindi na maharage ulichowahi kuuza?


Shahidi:Gunia 200,300 sijawahi kuzidisha




Wakili:Haumiliki kampuni


Shahidi:Ni kweli 



Wakili:Hauna hata leseni 


Shahidi:Biashara ninayofanya mimi haihitaji leseni



Wakili:Kwa hiyo hauna 


Shahidi:Eeh



Wakili:Kwa hiyo haulipi kodi


Shahidi:Ninalipa  ushuru



Wakili:Wapi


Shahidi:Sokoni



Wakili:Hauwezi kulipa ushuru sokoni wa gunia 200


Shahidi:Siwezi kuuza zote kwa pamoja



Wakili:iyo biashara ni ya kwako personal?


Shahidi:Tulikuwa tunafanya pamoja na Sabaya ila mimi ni msimamizi



Wakili:Kwa hiyo na Sabaya alikuwa anafanya biashara bila leseni?



Shahidi:Nimeshasema kwa aina ya biashara na mfumo tunaotumia hauhitaji kuwa na leseni




Wakili:Hizo biashara zenu za mahindi na maharage mmeanza mwaka gani


Shahidi:2018 



Wakili:Mmeshatengeneza kiasi gani?


Shahidi:Siwezi kujua kwa sababu ni fedha ambayo iko kwenye mzunguko



Wakili:Kwa biashara hii ambayo mimi naiona ni ndogo sana mtaji wenu ulikuwa kiasi gani?


Shahidi:Siwezi kujua manake fedha ziko kwenye mzunguko



Wakili:Wakati mlipoanza 2018


Shahidi:Milioni tatu



Wakili:Jesca unakubaliana na mimi biashara yenu ni ndogo sana labda uniambie mtaji wenu?


Shahidi:Nimesema fedha ziko kwenye mzunguko 



Wakili:Umeshawahi kufanya assesment ya biashara?


Shahidi:Sikumbuki



Wakili:Umesema umekaa na Sabaya na miaka minne?


Shahidi:Mitano sasa inakuwa 



Wakili:Mitano mingi,Sabaya hana kampuni


Shahidi:Ni kweli



Wakili:Hakuna biashara nyingine wewe na Sabaya zaidi ya mahindi na maharage?


Shahidi:Tunafanya ufugaji ambapo kwenye kufuga tunauza pia



Wakili:Ulisema mnafuga nini 


Shahidi:Ng'ombe, kuku na mbuzi



Wakili:Wewe na Sabaya mna kuku wangapi?


Shahidi:Mara ya mwisho niliwahesabu wako 600



Wakili:Wako wapi?


Shahidi:Wako Malula



Wakili:Mna ngonbe wangapi?


Shahidi:Mimi sijawahi kuwahesabu Lengai ndiyo anawahesabu



Wakili:Wewe ni mke wa Sabaya na haujui ngombe wake


Shahidi:Yeye ndiyo anapenda kuhesabu



Wakili:Umewahi kuuza ngombe lini?


Shahidi:Mdiyo mwaka jana mwezi wa nane



Wakili:Mwaka jana umeuza wa ngapi?


Shahidi:Lengai ndiyo anajua 



Wakili:Wewe ni mke ng'ombe zinauzwa haujui idadi?


Shahidi:Nataka kujua kilichopatikana 



Wakili:Mwaka juzi 2020 Sabaya aliuza ngombe wangapi


Shahidi:Sijui



Wakili:Haujawahi kujui Sabaya ameuza ngombe wangapi mwaka 2020?


Shahidi:Sifahamu 



Wakili:2019


Shahidi:Sifahamu



Wakili: 2018


Shahidi:Sifahamu



Wakili:Umesema hautaki kujua idadi unataka kujua kiasi mwaka jana alipata kiasi gani?


Shahidi:Mwaka jana hapana hakuuza



Wakili:Mwaka 2020 alipata kiasi gani kwa kuuza ng'ombe?


Shahidi:Kwa hela aliyokuja nayo 2020 ilikuwa Milioni 20 



Wakili:Katika mauzo hayo ingawa wewe ulikuwa hauzingatii idadi ya mifugo mlikuwa mnalipa kodi?


Shahidi:Tulikuwa tunalipa ushuru mnadani



Wakili:Sabaya alikuwa ana chanzo kingine cha mapato?


Shahidi:Mshahara 



W mbuzi anao wangapi


S sijawahi kuhesabu



Wakili:Nani anachunga mbuzi na ngombe huko shamba?



Shahidi:Kuna watu wako huko shamba 



Wakili:Shamba la nani?


Shahidi:La kwetu



Wakili:La  wewe na Sabaya


Shahidi:Ndiyo



Wakili:Shamba la heka ngapi Jesca?


Shahidi:11



Wakili:Umesema wewe na Sabaya mnamiliki magari mangapi?


Shahidi:Mawili namba T 341 ANT na T 222 BDY



Wakili:Gari la tatu


Shahidi:Ni hayo tu ninayoyafahamu




Wakili:Hiyo T 341 ATN ilinunuliwa ukiwa kwenye ndoa? 


Shahidi:Ndiyo



Wakili:Na hii T 222 BDY ilinunuliwa ukiwa kwenye ndoa?


Shahidi:Ndiyo 



Wakili:T 222 BDY mliinunua kwa Sh.milioni 60?


Shahidi:Hapana, tuliinunua kwa kuvunja unatoa gari unajazia hela  kidogo unachukua gari



Wakili:Na wewe Sabaya unampenda sana ndiyo mana unahudhuria kesi yake?


Shahidi:Kwa ajili ya kujua mwendelezo wa kesi si kumpenda 



Wakili:Ndiyo mana nakuona hapa tena 


Shahidi:Kujua mwendelezo wa kesi



Wakili:Shahidi wa 12 ulimsikia hapa mahakamani si ulikuwepo na ulimsikia


Shahidi:Ndiyo



Wakili:Pole lakini mume wako anashitakiwa umekuwa mwaminifu kuwasikikiza mashahidi wote 


Shahidi:Ndiyo



Wakili:Shahidi Sabri alisema gari T 222 BDY walimuuzia Sabaya na ulitolewa mkataba wa mauziano wa lile gari kama kielelezo 


Shahidi:Ndiyo



Wakili:Ule ndiyo mkataba wenyewe?


Shahidi:Mkataba wenyewe nimeutoa mimi na si ule 



Wakili:Kadi ya gari namba T 222 BDY inasomeka jina la Sabaya na si la kwako


Shahidi:Ndiyo



Wakili:Na hilo lingine?


Shahidi: Linasomeka jina la kwangu



Wakili: Alikununulia Sabaya


Shahidi: Tulinunua pamoja


Kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho Januari 18, shahidi huyo atakapoendelea kuhojiwa na mawakili wengine wa Serikali.