Mpango usafirishaji wa dharura wazazi, watoto wachanga wazinduliwa Arusha

Arusha. Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wamezindua mpango wa usafirishaji wa dharura za wazazi na watoto wachanga mkoa wa Arusha ujulikanao kama m-mama  ambao utawezesha kurahisisha upatikanaji wa huduma ya mama na mtoto  kutoka kituo kimoja kwenda kingine kwa wakati.
Akizungumza  jijini Arusha wakati wa uzinduzi huo uliofanyika katika hospitali ya rufaa ya mkoa Mt Meru, Mkuu wa kanda ya kaskazini Vodacom, George Venanty amesema kuwa mpango huo utasaidia sana kuokoa vifo vitokanavyo na mama na mtoto.
Amesema kuwa, Vodacom wamekuwa washiriki katika mradi huo katika  kuhakikisha kuwa kunakuwepo na mafanikio na kuweza kupunguza vifo vya wakinamama .

Aidha Venanty amesema uwepo wa mfumo huo unaweza kuondoa changamoto ya ufinyu wa  magari ya wagonjwa (ambulance) uliopo kwani watakuwa wanatumia magari ambayo yapo kwenye mfumo kwa muda wowote ambayo tayari yalishaandaliwa kwa kazi hiyo.


"Wahudumu wa afya watumie mfumo huo kuhakikisha wanaokoa vifo vya wanawake na watoto wachanga hivyo naomba sana mchukulie  kwa uzito ili uweze kufanikiwa kwani mfumo huu tayari tumeuzindua katika mkoa wa Manyara  na hadi kufikia Septemba mwaka huu tutakuwa umefika mikoa yote," amesema Venanty

Muuguzi Mkuu wa mkoa na Mratibu wa mpango wa m-mama kwa mkoa wa Arusha, Getrude Anderson  amesema ni mpango wa usafirishaji kwa wakina mama wajawazito ambao wanapata dharura na kuweza kuhamishwa kutoka  kituo kimoja kwenda kingine.

"Endapo akitokea mgonjwa ambaye amepata dharura  wakati wa kujifungua  wanaangalia gari ambayo ipo karibu kwani  tayari walishaingia  mkataba na madereva mkoa mzima hivyo wanachofanya  ni kuchagua  gari na kufika kituo  kilicho  karibu na kuweza kutoa huduma ya haraka kwenda kituo kingine," amesema.

Amesema kuwa, uwepo wa huduma hiyo unarahisisha  kwa kiwango kikubwa sana kwani badala ya gari kutembea  umbali wa kilometa  mia mbili inatembea  umbali  wa kilometa  mia moja tu .

"Nawaomba sana watumishi tuutumie mfumo huu kwani utaweza kuokoa maisha ya mama na mtoto na kuwezesha upatikanaji wa takwimu sahihi za wakinamama "amesema Getrude.

Ofisa elimu wa mkoa wa Arusha, Abel Ntupwa akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Arusha, amesema mfumo  huo  utaleta suluhishi la changamoto ya upatikanaji wa usafiri wa dharura kwani ambulance za serikali zilizopo hazitoshi.


Aidha amesema mpango huo utaongeza hali ya furaha  na kujiamini kwa wanawake na hivyo ni vizuri kila Mtanzania  akafikiwa  na huduma hiyo kwani ni ubunifu wa hali ya juu hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha anaunga mkono mpango huo.