Mtoto achomwa mikono Mtwara akidaiwa kuiba Sh1, 000

Mtoto achomwa mikono Mtwara akidaiwa kuiba Sh1, 000

Muktasari:

  • Mkazi wa Kijiji cha Ndumbwe Wilaya ya Mtwara, Hamis Mmalala amemchoma moto vidole vya mikono mtoto wake, Bashiru (10) baada ya kumtuhumu kuwa ameiba Sh1,000 iliyokuwa imeandaliwa kwaajili ya kununua vitafunwa.

Mtwara. Mkazi wa Kijiji cha Ndumbwe Wilaya ya Mtwara, Hamis Mmalala amemchoma moto vidole vya mikono mtoto wake, Bashiru (10) baada ya kumtuhumu kuwa ameiba Sh1,000 iliyokuwa imeandaliwa kwaajili ya kununua vitafunwa.


Akizungumza na Mwananchi Digital iliyofika nyumbani kwake kufuatilia tukio hilo, Mmalala alisema kuwa moto huo aliuwasha kwa nia ya kumtisha mtoto ili aachane na vitendo vya udokozi akidai halikuwa lengo la kumunguza.


Amedai kuwa haikuwa lengo lake kumuuimiza mtoto wake bali ilikuwa ni bahati mbaya ambapo na yeye aliungua katika harakati za kutaka kuuzima moto huo.


“Mtoto aliungua bahati mbaya huyu mtoto anatabia ya udokozi hata unga anaiba anaficha hapo nyumbani kuna mtama sijui aliiba wapi siku ile nilikuwa namtisha lakini bahati mbaya nikamuunguza mkono nikamsaidia kuuzima moto lakini napambana nitibu “

“Sikuwa na nia mbaya ningetaka kumdhuru ningemdhuru siku nyingi lakini ilikkuwa ni kama kumtisha tu sikudhani kama ungewaka sana hata hivyo hiki nilichofanya sio sawa ndio maana nikasema kuwa bahati mbaya ndio uwezo ukanishinda natafuta pesa ili nimpeleke Hospitali” alisema Mmalala
Naye mtoto Bashiru alisema kuwa tukio la kuiba Sh1000 alisingiziwa.


“Baba alinichoma moto nyuma ya nyumba alinifunga na nyasi na kuanza kunichoma moto kwenye vidole baada ya kunituhumu kuwa nimeiba pesa ya dada Sh1000 pamoja na kulia sana lakini hakuniachia baadae aliuzima na hakuniwekea dawa yoyote nilishuhudia maji yakitoka kwenye vidole vilivyoungua” alisema mtoto huyo huku akionyesha vidole ambavyo vimeungua.


 “Inapofika wakti wa kula nakaa pembeni tu wao nakazi ya kunikatia ugali na kuniwekea kwenye kiganja ndio nakula siwezi kufanya kitu chochote nimeungua vidole vinne vya mkono mmjoa huku mkono mwinigne kikiungua kidogo kimoja siwezi hata kujisadia mwenyewe nasaidiwa na watu” alisema Bashiru

Zainabu Nachimo ambaye ni mama wa kambo wa Bashiru alisema kuwa wakati mtoto huyo anachomwa mikono yeye alikuwa shambani ambapo baada ya kurejea alikuta taarifa hizo.

“Juzi tulipata mgeni ambaye ni dada yake na Bashiru alitunza pesa yake Sh1400 lakini alitumia 400 ikabaki 1000 asubuhi wanataka kwenda kununua vitafunwa hawakuiona lakini walidhani ni Bashiru ndiye kaichukua”
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kitongoji cha Namivangu kuijiji cha Ndumbwe, Hamis Mitandi alisema kuwa alichelewa kupata taarifa hizo za mtoto kuchomwa moto.

“Hili tukiio sikulijua mapema laiti ningejua ningelifanyia kazi mapema kwakweli nimesikitishwa na mtoto huyu kupata majeraha kama haya pamoja na kumfahamu kwa muda mrefu sijawahi kuona akifanya matukio kama haya”

Huyu mtoto anahitaji malezi mazuri na miongozo ili baadae aweze kuwa msaada katika jamii yake sijawahi kupata taarifa yake yoyote ya kufanya ukatili wowote hili ni la kwanza tutamsaidia mtoto apate matibabu” alisema Mitandi

Akitolea ufafanuzi wa matukio kama hayo Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara, Mark Njera alisema kuwa kuna kesi mbili za watoto kujeruhiswa na wazazi na wazazi wameshakamatwa.

“Vyanzo vya matukio hayo ni vitu vya ajabu mtoto wa kwanza alikula ugali na nyama akachomwa mikono yake lakini mtoto wa pili ameiba Shilingi 1000 hii sio sawa inaonyesha wazi kuwa elimu kwa jamii sisi tunafanya kwa nafasi yetu lakini tunayojamii masikini ni tatizo kubwa kama hatutatoa elimu kwa jamii” alisema Njera