Mwanzilishi wa Precision Air Kuzikwa Rombo Jumatano
Muktasari:
- Mwili wa Mwanzilishi na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Shirika la Ndege la Precision Air, Michael Ngaleku Shirima (80) unatarajiwa kuzikwa siku ya Jumatano Juni 14, mwaka huu Wilaya ya Rombo, Mkoani Kilimanjaro.
Moshi. Mwili wa Mwanzilishi na Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya Shirika la Ndege la Precision Air, Michael Ngaleku Shirima (80), unatarajiwa kuzikwa siku ya Jumatano Juni 14, mwaka huu Wilaya ya Rombo, Mkoani Kilimanjaro.
Shirima alifariki dunia Juni 9, 2023 wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam baada ya kulazwa siku ya Juni 8.
Kufuatia msiba huo, Rais Samia Suluhu Hassan ametuma salamu za pole kwa familia hiyo na kusema baada ya utumishi wake wa umma, kwa zaidi ya miaka 30 amekuwa sehemu muhimu katika biashara ya anga na shughuli za kijamii katika nchi.
Akizungumza na Mwananchi, Msemaji wa familia hiyo, Abdallah Singano amesema mwili wa mzee Shirima utasafirishwa siku ya Jumatatu kutokea Dar es Salam kwenda nyumbani kwake jijini Arusha ambapo watatoa nafasi kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki kuaga mwili wa mpendwa wao.
"Kwa sasa tupo Dar es Salam, lakini msiba upo Arusha, tunategemea kusafirisha mwili siku ya Jumatatu kutoka Dar es Salam kwenda Arusha, ambapo Arusha tutatoa nafasi kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki kuaga mwili alafu tutaondoka kwenda Tarakea, Rombo siku ya Jumanne na Jumatano tutampumzisha katika nyumba yake ya milele,"