Ndugai: Serikali iangalie upya ujenzi Bandari ya Bagamoyo

Ndugai: Serikali iangalie upya ujenzi Bandari ya Bagamoyo

Muktasari:

Spika wa Bunge, Job Ndugai ametaka Serikali kuangalia upya mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo mkoani Pwani na iwapo ni jambo jema waendelee nao.

Dodoma. Spika wa Bunge, Job Ndugai ametaka Serikali kuangalia upya mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo mkoani Pwani na iwapo ni jambo jema waendelee nao.

Ndugai ameeleza hayo leo Alhamisi Aprili 8,2021 bungeni mjini Dodoma katika mjadala wa mpango wa tatu wa maendeleo ya Taifa wa miaka mitano (2021/2022 hadi 2025/2026).

“Nawapongeza sana kamati ya bajeti kuona kama mradi wa Bandari ya Bagamoyo unaweza kufikiriwa. Mimi nilisema niliwahi kusafiri katika safari ya Bunge  tulienda katika mambo ya Bunge mtandao kule,” amesema Ndugai.

Amesema katika safari hiyo alikutana na bodi ya kampuni ambayo ilitaka kujenga mradi huo iliyowasilisha taarifa iliyokuwa na ushawishi mkubwa.

Amesisitiza kuwa hata Waziri wa Fedha na Mipango,  Dk Mwigulu Nchemba akimpa nafasi anaweza kuzikumbuka hoja zilizowasilishwa na kampuni hiyo, “viongozi wetu hawawi brief sawasawa. Kuna watu wanawadanganya viongozi kabisa. Kiongozi akishasema wote mnanyamaza lakini hapa mnaona amekuwa mislead (amepotoshwa).”

Amesema kiongozi mkubwa wa kampuni hiyo ambaye hakumtaja jina aliwaeleza kuwa Tanzania ni marafiki wakubwa na kwamba wanaufanya mradi huo wakijua kuwa ni nchi marafiki wa China.

Ndugai akimnukuu  kiongozi huyo amesema alimueleza kuwa kwenye kampuni hiyo wanaajiriwa  vijana ambao hawaijui vyema Tanzania ndio maana wazee wameamua kuusimamia mradi huo.