Nusrat Hanje: Siasa ni fursa lakini lazima upambane

Nusrat Hanje: Siasa ni fursa lakini lazima upambane

Muktasari:

  • Nusrati Hanje anasema alianza kujihusisha na siasa akiwa bado mwanafunzi wa chuo kikuu mwaka 2010, pale alipojiunga na Chadema kwa kuwa alipenda siasa za upinzani.

Nusrati Hanje anasema alianza kujihusisha na siasa akiwa bado mwanafunzi wa chuo kikuu mwaka 2010, pale alipojiunga na Chadema kwa kuwa alipenda siasa za upinzani.

Anasema kwenye siasa hakuna kitu rahisi, unatakiwa uwe na ngozi ngumu kwa sababu kwanza kuna fursa za kisiasa.

Lakini sehemu yenye fursa kuna pilikapilika nyingi, kuna kuvunjana moyo, kurudishana nyuma, kuna kubeba[1]na kwa namna moja ama nyingine.

Hii yote ni kwa sababu huko kuna fursa. “Hata hivyo, mimi ninajiamini kuwa ninao uwezo wa kufanya jambo kubwa kwenye siasa, siwezi kufananishwa na baadhi ya wanaoamini katika kubebwa.” Ndivyo anavyoeleza mbunge wa Viti Maalumu, Nusrati Hanje jinsi alivyokumbana na vikwazo katika safari yake ya kisiasa hadi alipofikia.

Hata hivyo, ikumbukwe kuwa Hanje ni miongoni mwa wabunge 19 wa Viti maalumu walioko bungeni waliovuliwa uanachama na chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa madai ya kuingia bungeni kinyume cha utaratibu wa chama hicho.

“Mimi nilikuwa naamini katika upinzani sana kwa sababu naamini katika fikra mbadala, lakini haimaanishi kwamba chama tawala hakina watu wenye fikra mbadala, yaani watu ambao wanazungumza masuala yanayogusa watu,” anasema Hanje katika mahojiano maalumu na Mwananchi yaliyofanyika Jijini Dodoma hivi karibuni.

Alikuwa akizungumzia safari yake kisiasa na changamoto alizokutana nazo kwa kuwa aliingia akiwa bado binti mdogo.

“Lakini, kwenye kufanya siasa mimi mwenyewe nimependa kwa sababu naamini ninatakiwa niwe sehemu ya utatuzi wa matatizo ya jamii.

Na wanasiasa ni watatuzi wa matatizo katika jamii, nikaona namna pekee ni kuingia kwenye siasa.

“Lakini kwa mapenzi yangu na utashi wangu, nikaingia upinzani ambako pia siyo kurahisi kwa sababu, kwanza hakuna rasilimali za kutosha, hasa fedha hali inayowafanya wengi wajitolee katika kukiwezesha chama kisonge mbele,” anasema Hanje.

Uzoefu wake Hanje anasema kwenye siasa hakuna kitu rahisi. “Mimi nasema uwe mkali, unatakiwa uwe na ngozi ngumu kwa sababu kwanza, kuna fursa za kisiasa na sehemu yenye fursa kuna pilikapilika nyingi, kuna kuvunjana moyo,kurudishana nyuma na kubebana kwa sababu kuna fursa.

Anasema kinachohitajika ni kuangalia nani anakuthamini na hiyo haihitaji mtu kuwa na shahada ya uzamili.

“Unatakiwa kujua kuna kupambana kwenye vyama vya siasa, hasa ukiwa huna mtu wa kukushika mkono, utendaji wako ndiyo ukutetee,” anasema Hanje.

Utabiri wa baba yake Anasema baba yake alifariki dunia wakati yeye akiwa kidato cha tatu na alikuwa hajajipambanua kwamba ataingia kwenye siasa.

“Ila alikuwa akisema naweza kuwa kiongozi kwa sababu nilikuwa napata mrejesho kutoka kwa marafiki zake akizungumza kwamba naweza kuwa kiongozi, hata kama mimi sipo huyu (Nusrati) anaweza kuchukua nafasi yangu kama mimi kwenye familia,” alisema.

Maneno ya baba yake yanathibitishwa na alivyoweza kuongoza na kupigania haki za wadogo zake baada ya wazazi wao kufariki dunia. Kitendo chake cha kuandika barua kukataa familia isiteue msimamizi wa mirathi hadi yeye atakapotimiza umri wa miaka 18, kilionyesha alivyokuwa tayari kuwa kiongozi

Harakati za kisiasa Hanje ambaye kitaaluma ni mwalimu, anasema mwaka 2015 aliacha kazi ya ualimu akaenda kuweka nia Chadema ya kugombea ubunge wa jimbo la Kigam[1]boni. “Tulikuwa wagombea sita, lakini nilikuwa wa tatu. Na nilikuwa na umri wa miaka 25,” anasema.

Anasema katika wagombea wote yeye ndiye alikuwa mwenye umri mdogo. “Sikufanikiwa nikaingia kwenye timu ya kampeni ya Taifa ya kumnadi (Edward) Lowassa.

Nikazunguka nchi nzima kufanya siasa wakati huo nili[1]kuwa katibu wa vijana wa jimbo la Kigamboni. “Baada ya uchaguzi nikarudi kufundisha shule nyingine. Baadaye nikabanwa na masuala ya chama, nikaacha tena kufundisha,” anasema. Anasema aliwahi pia kuwa mwenyekiti wa vijana wa wilaya wa Chadema, katibu mkuu wa vijana wa Taifa na pia ni mjumbe wa kamati kuu ya chama.

“Hakukuwa na katibu mkuu wa vijana mwanamke tangu Chadema imeanzishwa, kwa hiyo kwangu ilikuwa ni mafanikio makubwa na iliwavutia vijana wengine wa kike waliokuwa wanatamani kuwa wanasiasa.

“Ndio tukaanzisha ‘Bavicha Queens’, mabinti wa Baraza la Vijana la Bavicha, lengo lilikuwa ni kutengeneza jukwaa la kuwajengea uwezo vijana wa kike.

“Nilianzisha mchakato wa kuandika sera ya vijana ya Chadema ambao ni mbadala wa sera ya vijana ya taifa,” alisema.

Ngono kwenye siasa Hanje alizungumzia namna alivyopambana na changamoto za kuhusishwa na uhusiano wa kimapenzi ndani ya Chadema na namna alivyozichukulia tuhuma hizo.

“Siyo siri vyama vya siasa vina kashfa sana ya ngono ndani, siyo Chadema peke yake, ni vyama vya siasa vyote, sehemu yoyote ambayo kuna mchanganyiko wa watu suala kama hili lazima litajitokeza tu, sasa hapo ni hiari ya mtu kuamua kutenda ama kuepuka.

Kwa hiyo kusingiziwa kwamba natembea na mtu fulani ni kitu ambacho kilinikatisha tamaa.

Nikawa najiuliza yaani mtu haoni uwezo wangu utaonekana pale nitakapokubali kuvua nguo. Nikasema hili hapana. “Mimi siwezi kukubali kufanyiwa ukatili kama huu eti kwa sababu tu mtu anataka kunilazimisha kuwa na uhusiano wa ili anipatie nafasi, hapana,” anasema Hanje.