Nyati mwingine mweupe aonekana Tarangire

Muktasari:

Nyati mwingine mweupe ameonekana katika hifadhi ya Taifa ya Tarangire na kuvutia watafiti na watalii kujua aina hii mpya ya wanyama hao watalii wengi waliokuwa hifadhini kuanza kumfatilia.

Tarangire. Nyati mwingine mweupe ameonekana katika hifadhi ya Taifa ya Tarangire na kuvutia watafiti na watalii kujua aina hii mpya ya wanyama hao watalii wengi waliokuwa hifadhini kuanza kumfatilia.

Akizungumza na Mwananchi mmoja wa mashuhuda wa nyati huyo, Jeremiah Peter amesema nyati huyo ni mkubwa tofauti na nyati wengine katika hifadhi hiyo na amekuwa akikaa katikati ya nyati wengine.

"Haya ni maajabu mengine katika Utalii wa Tanzania tunaimani huyu nyati atavutia watalii"amesema

Kamishna Msaidizi Mwandamizi Mawasiliano wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Taapa) Pascal Shelutete alisema nyati huyo ameonekana kwa mara ya kwanza na ni kuvutio.

Hata hivyo alisema uchunguzi wa awali unaonesha huenda nyati huyo ni albino sawa na wanyama wengine weupe waliowahi kuonekana katika hifadhi hiyo akiwepo twiga.

"Tutaendelea kumfatilia na kumtunza nyati huyo kwani tangu habari zake zimejulikana kuna wengi wameanza kufatilia" amesema.


Nyati mwingine mweupe jike alivyoonekana


Kuonekana nyati mwingine mweupe jike jana kumeanza kuibuwa hisia tofauti kwa watafiti kwenda Tarangire kuchunguza zaidi kulikoni.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumapili Mei 22, 2022 Mtafiti Mwandamizi wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori nchini (Tawiri), Dk Edward Kohi amesema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa nyati hao weupe ni albino.

Hata hivyo jamii ya Masai ambao wamezunguka hifadhi hiyo wanaeleza nyati hao weupe kuonekana sasa ni ishara nzuri ya kukuza utalii na hawaamini kama ni albino.

Long'oi Mollel anasema nyati weupe ni ishara nzuri kukua utalii Tarangire kwani hata wao licha ya kuishi katika eneo hilo hawajawahi kuwaona nyati weupe.

"Hii ni baraka kubwa na inaonesha utalii kukuwa Tarangire na sisi wamasai wahifadhi wa asili tutalinda hawa nyati kwani wanaishi katika vijiji vyetu na mimi nadhani sio albino ni Mungu kaleta aina hii Kwani tangu wadogo hawajaonekana" amesema