Othman akumbusha mshikamano akitambuliwa kwa wanachama
Muktasari:
- Mjumbe wa kamati kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo, Othman Masoud Othman amewataka wanachama wa chama hicho kushikamana ili kutimiza malengo yaliyokusudiwa ikiwamo ya kudumisha umoja.
Unguja. Mjumbe wa kamati kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo, Othman Masoud Othman amewataka wanachama wa chama hicho kushikamana ili kutimiza malengo yaliyokusudiwa ikiwamo ya kudumisha umoja.
Othman ambaye pia ni makamu wa kwanza wa rais Zanzibar ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Mei 29, 2021 Wilaya ya Kaskazini A Unguja katika kikao cha kumtambulisha kwa viongozi na wafuasi wa chama hicho.
Amebainisha kuwa umoja na mshikamano uliopo katika chama hicho ndio uliokipa nguvu na heshima Zanzibar na Tanzania Bara.
“Wazee wetu walisema umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu, mshikamano huo ndio uliopelekea uimara wa chama. Kwa sababu ya mshikamano wetu hatuyumbi katika kudai haki pamoja na mamlaka ya Zanzibar ndani ya Tanzania na nje ya Tanzania, ”amesema Othman.
Huku akieleza jinsi wanaojiunga na chama hicho wanavyovutiwa na mshikamano wao, Othman amewataka wanachama wa ACT-Wazalendo kutouchezea mshikamano huo huku akiwataka kuenzi yaliyofanywa na aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho, Hayati Maalim Seif Sharif Hamad.
“Tunalopigania tuendeshe nchi yetu kistaarabu pasina mtu yoyote kupata madhara wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi kwani tuna haki ya kuishi kwa amani katika nchi yetu.” Amesema.
Akimtambulisha Othman, makamu mwenyekiti wa chama hicho, Juma Duni Haji amesema, “leo ninakutambulisha kwa viongozi wa mikoa ninachokuomba usikae nyuma tuanze kazi ya kujenga chama na kupigania haki za Wazanzibari.”