Rais azindua kiwanda kikubwa cha nyama Longido
Muktasari:
- Rais Samia Suluhu amezindua kiwanda kikubwa cha chama kilichopo katika Wilaya ya Longido Mkoa Arusha chenye thamani ya Sh17 bilioni.
Arusha. Rais Samia Suluhu amezindua kiwanda kikubwa cha chama kilichopo katika Wilaya ya Longido Mkoa Arusha chenye thamani ya Sh17 bilioni.
Kiwanda hicho cha Eliya Food Overseas Ltd, kimejengwa Katika eneo la mauzo ya nje (EPZ) iliyotolewa na Mamlaka ya EPZA na ujenzi wa kiwanda hiki ulikamilika Novemba 2020, na uzalishaji ulianza Desemba 2020.
Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika leo Jumatatu, Octoba 18 ,2021 Rais Samia amesema ni fursa Kwa wafugaji wa Wilaya ya Longido na Mkoa wa Arusha kuuza nyama .
Amesema kiwanda hicho kitakuwa kikisafirisha nyama nje ya nchi hivyo hivi sasa soko la mifugo ni la uhakika.
Awali Mkurugenzi wa kiwanda hicho, lrfhan Virjee amesema kiwanda hicho kina uwezo wa kuchakata tani 20 za nyama ya ng'ombe na tani 20 za nyama ya mbuzi na kondoo.
"kwa sasa kiwanda hiki kinafanya kazi kwa asilimia 30 ya uwezo wa kuchinja na kuchakata nyama kwa mifugo ya mbuzi na kondoo na asilimia 10 kwa mifugo ya ng'ombe"amesema
Amesema lengo la kiwanda hicho ni kufikia uzalishaji wa asilimia 80 kufikia mwishoni mwa mwaka 2021 na kukuza masoko mapya ya bidhaa zetu
Amesema mpaka sasa kiwanda kimeshatoa ajira 150 za moja kwa moja kwa Watanzania ambao ni madaktari watatu wa wanyama kutoka serikalini wanaofanya kazi za ukaguzi wa afya na ubora wa mifugo hapo kiwandani.
Awali Waziri wa Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo amesema kiwanda hicho ndio kikubwa kwa sasa hapa nchini kati ya viwanda 10 vilivyopo nchini.
Profesa Mkumbo amesema kiwanda hicho kwa Sasa ni kati ya viwanda vikubwa 618 vilivyopo hapa nchini.