Rais Falme za Kiarabu (UAE) afariki

Muktasari:

  • Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan amefariki leo Ijumaa akiwa na umri wa miaka 73 baada ya kuugua kwa muda mrefu,  vyombo vya habari vya serikali vimesema.


Abu Dhabi, UAE (AFP). Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan amefariki leo Ijumaa Mei 13, 2022 akiwa na umri wa miaka 73 baada ya kuugua kwa muda mrefu,  vyombo vya habari vya serikali vimesema.


Nafasi ya rais huyo wa taifa lenye utajiri wa mafuta na ambaye amekuwa haonekani hadharani mara kwa mara, inawezekana ikachukuliwa na kaka yake ambaye ni mrithi wa falme ya Abu Dhabi, Prince Mohammed bin Zayed, ambaye tayari ameshaonekana kuwa ndiye mtawala wa UAE kabla ya kutangazwa rasmi.


"Wizara ya masuala ya rais inawatangazia wananchi wa UAE, mataifa ya Kiarabu na Kiislamu na dunia kwa ujumla kifo cha Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan," shirika la habari la WAM liliandika katika akaunti yake ya Twitter.


Wizara hiyo ilitangaza siku 40 za maombolezo na kwamba bendera zitapepea nusu mlingoti kuanzia leo Ijumaa na kazi kusimamishwa katika ofisi za umma na binafsi kwa siku tatu.


Sheikh Khalifa alichukua madaraka Novemba mwaka 2004 akiwa rais wa pili, akimbadili baba yake kama kiongozi wa 16 wa Abu Dhabi, ambayo ni dola tajiri kulinganisha na nyingine katika shirikisho hilo lenye falme saba.


Amekuwa akionekana kwa nadra hadharani tangu mwaka 2014, wakati alipofanyiwa upasuaji baada ya kupata kiharusi, ingawa aliendelea kutoa maamuzi. Sababu za kifo chake hazikutolewa mara moja.


Taifa la UAE, ambalo lilikuwa chini ya usimamizi wa Uingereza na ambalo lilianzishwa mwaka 1971, limetoka katika hali ya jangwa na uchumi wake kukua katika historia yake ya muda mfupi, ikinufaika na utajiri wa mafuta na kuibuka kwa Dubai kuwa kituo cha biashara na kifedha.


Taifa hilo, ambalo ni la pili kwa kuwa na uchumi mkubwa baada ya Saudi Arabia, pia limeibukia kuwa na nguvu ya kisiasa, likiziba nafasi iliyokuwa inashikiliwa na nchi kama Misri, Iraq na Syria.