Rais Samia aeleza umuhimu ujenzi kituo cha forodha

Muktasari:

  • Rais Samia Suluhu Hassan ameeleza lengo la ujenzi wa kituo cha pamoja cha forodha kati ya Tanzania na Malawi  ni kuhakikisha usalama wa watu  na bidhaa zinazoingizwa nchini.

Kyela. Rais Samia Suluhu Hassan ameeleza lengo la ujenzi wa kituo cha pamoja cha forodha kati ya Tanzania na Malawi  ni kuhakikisha usalama wa watu  na bidhaa zinazoingizwa nchini.

Rais Samia amesema hayo  leo Jumapili Agosti 7, 2022  wakati akizindua  mradi unaotekelezwa na  Wakala wa  Barabara Tanzania (Tanroad) uliojengwa katika kata ya Njisi Kasumuru Wilaya ya Kyela ambao umefikia asilimia 87 .

Amesema  lengo la ziara yake  ya siku nne mkoani Mbeya ni  kukagua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali hususan kituo hicho na kuhimiza usalama wa watu na bidhaa  uimarishwe sambamba na kuhakikisha  bidhaa zinazoingizwa nchini zinalipiwa.

Samia amesema  licha ya kuweka jiwe la msingi amefurahishwa na mapokezi ya wananchi wa Kyela  na kutoa fursa kwa mbunge wa Kyela, Ally Mlaghila kueleza changamoto ili kuzitafutia majibu.

Akizungumza na Mamia ya wananchi wa Kyela, Mlaghila amemshukuru Rais Samia kwa kuwapatia Sh800 milioni i kwa ajili ya mradi wa maji katika maeneo yenye changamoto.

Mlaghila  alimuomba Rais kupitia  mto Songwe unaotenganisha nchi ya Tanzania na Malawi,  kuwepo kwa mradi wa kilimo cha umwagiliaji kutokana na changamoto za mafuriko zinazosababisha mpaka baina ya nchi hizo kutoeleweka  .

''Mama tunaomba tusaidie mto huu utumike kuanzisha mradi wa kilimo cha umwagiliaji kwani yanapotokea mafuriko kuna shida sana kwa wananchi wangu  makazi yao kuhama mara kwa mara mara kuwepo Tanzania mara Malawi," amesema.

Mtendaji nkuu  wa Tanroad, Rogatus Mativila amesema mradi huo umekamilika kwa asilimia  zaidi ya 87 licha ya kuwepo kwa changamoto huku akieleza kuwa chachu ya kukuza mapato ya serikali.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera amemuomba Rais Samia  kusaidia kupatikana  kwa gari la zimamoto kutokana na ukubwa wa mkoa huku akigusia kituo hicho kwamba kitaongeza  mapato ya Serikali kutokana na watu wa nchi jirani ya Malawi kutegemea manunuzi ya bidhaa nchini Tanzania kwa kupitia mpaka wa Kasumuru Wilaya ya Kyela.

Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson aliwataka wananchi wa Kyela kujitokeza kwenye zoezi la sensa ya watu na makazi ili kumrahisishia Rais Samia   katika kuboresha miradi ya maendeleo na mahitaji ya Watanzania.

Waziri wa Ujenzi na  Uchukuzi, Makame Mbarawa, amesema  wamepokea maagizo yote yaliyotolewa na Rais  Samia na yanaanza kufanyiwa kazi.

Mkazi  wa Njisi Kasumuru, Johnson Ally  ameipongeza Serikali ya awamu ya sita kwa kujenga kituo hicho kwani kitakuwa chachu ya kukuza uchumi kutokana na mwingiliano wa shughuli za kiuchumi.