Rais Samia kuzindua ripoti miaka 10 ya THRDC

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan atazindua ripoti inayozungumzia hali ya watetezi wa haki za binadamu na asasi za kiraia nchini Tanzania kwa miaka 10.


Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan atazindua ripoti inayozungumzia hali ya watetezi wa haki za binadamu na asasi za kiraia nchini Tanzania kwa miaka 10.

Hayo yamesemwa leo Ijumaa, Mei 13, 2022 na Mratibu wa kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), Onesmo Olengurumwa wakati akifungua mkutano wa maadhimisho ya miaka 10 ya mtandao huo ulioanzishwa rasmi mwaka 2012.

“Ilikuwa safari ndefu, leo tunatarajia kuzindua taatifa yetu inayoonyesha miaka 10 tumefanya nini na tutafanya nini miaka 10 ijayo. Ripoti hii ina mambo mengi hasa kuhusu shughuli zilizowahi kufanya na mtandao na namna ilivyotoa mchango katika kushiriki masuala mbalimbali ya haki za binadamu,” amesema Olengurumwa.

Amesema pamoja na ripoti hiyo, pia kutakuwa na ripoti nyingine inayozungumzia hali ya utetezi wa haki za binadamu Tanzania mwaka 2021.

“Ripoti hii imeelezea hali ilivyokuwa kwa baadhi ya matukio ya haki za binadamu ikiwemo kesi, changamoto za ukiukwaji wa haki za binadamu, kesi tulizozishughulikia, waliokamatwa, waliofunguliwa kesi.

“Pia tumeweka taarifa za usalama wa waandishi wa habari, mauaji ya waandishi wa habari, vitisho na kuteswa kwa waandishi, ikiwemo mwandishi wa Mwananchi Jesse Mikofu kule Zanzibar,” amesema Olengurumwa.

Tume ya Haki za Binadamu imesema itakuwa bega kwa bega na THRDC katika kuhakikisha wanashirikiana kwa pamoja katika kulinda, kutunza na kutetea haki za binadamu.

Balozi wa Marekani, Donald Wright amesema mtandao huo ni muhimu kwa sababu unafanya kazi muhimu sana ya kulinda na kutetea haki za watu Tanzania.

“Tunaomba muendelee na kazi hii muhimu, tunahitaji msimamie haki za binadamu kwa ajili ya Watanzania pia kwa kusaidiana na Serikali,” amesema.