RC Kilimanjaro awatupia zigo mamlaka ya maji
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu akisoma maelezo kuhusu mradi wa maji wa Mkuu mjini na Kijiji Cha Ikuini wilayani Rombo unaotekelezwa na Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Rombo, utakaowanufaisha wananchi zaidi ya 14,000 wanaokabiliwa na shida ya maji. Picha na Janeth Joseph
Muktasari:
- Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu ameagiza Bodi ya maji ya bonde la pangani (Pbw), Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Rombo(Rombowasa) na Wakala wa maji vijijini(Ruwasa) kutumia wataalam wake kufanya tafiti za kina kutafuta vyanzo vya maji na kuvifanyia usanifu ili kukabiliana na upungufu maji wilayani Rombo.
Rombo. Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu ameagiza Bodi ya maji ya bonde la pangani (PBW), Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Rombo (Rombowasa) na Wakala wa maji vijijini (Ruwasa) kutumia wataalam wake kufanya tafiti za kina kutafuta vyanzo vya maji na kuvifanyia usanifu ili kukabiliana na upungufu maji wilayani Rombo.
Babu ametoa maagizo hayo wakati akiweka jiwe la msingi katika mradi wa maji wa awamu ya kwanza wa uboreshaji wa huduma ya maji katika kijiji cha Ikuini, wilayani humo wenye lita za ujazo 500,000 ambao unatakelezwa kwa gharama ya zaidi ya Sh192 milioni.
Babu amesema zipo juhudi zinazoendelea za kutafuta vyanzo vya maji katika maeneo ya Kilema na Kibosho ili miradi mingine mikubwa itakapopatikana iweze kunufaisha vijiji vilivyopo ukanda wa juu na kujengwa kwa wakati mwafaka.
"Hawa wataalamu wafanye hiyo kazi haraka iwezekanavyo, hatutaki malalamiko ya wananchi kuhusu maji maana fedha zipo, Mheshimiwa Serikali ina fedha, sitaki kuona tunakwamishwa kwa namna yoyote ile,"amesema RC Babu
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Rombowasa, Martin Kinabo amesema katika wilaya hiyo kunatekelezwa miradi mbalimbali ya maji ikiwemo miradi sita ambayo itagharimu zaidi ya Sh8 bilioni ambayo inaendelea na ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
"Mradi wa uboreshaji wa huduma katika kijiji cha Ikuini ni moja wapo ya miradi sita inayotekelezwa wilayani Rombo, mradi huu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo sehemu ya kwanza imetekelezwa kwa mfumo wa kutafuta mafundi wa eneo husika (force account),” amesema