Serikali: Ni mapema kupima manufaa ya Royal Tour

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imesema ni mapema kupima matokeo chanya ya filamu ya Royal Tour katika sekta ya utalii japo matumaini yaliyoanza kuonekana ni makubwa.

Dar es Salaam.  Serikali ya Tanzania imesema ni mapema kupima matokeo chanya ya filamu ya Royal Tour katika sekta ya utalii japo matumaini yaliyoanza kuonekana ni makubwa.

Pia, Serikali imesema inatarajia kufanya filamu nyingine kama hiyo hapo baadaye baada ya kufanya tathmini na kuchujua mkakati huo unachangia namna gani katika kutangaza na kukuza sekta hiyo nchini.

Filamu hiyo imezinduliwa mara tano ikiwamo awamu mbili nchini Marekani na mara tatu nchini huku viasharia kadhaa vya matumaini ya mchango wake yakianza kuonekana.

Kauli hiyo imetolewa leo Alhamisi Mei 11, 2022 na Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Hassan Abbasi wakati wa mkutano na waandishi wa habari Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo umeitishwa kwa ajili ya kueleza tathmini ya ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Uganda na Marekani.

“Manufaa ni ngumu kupima kwa sasa, ni muda mfupi sana lakini kuna matunda yameanza kuonekana baada ya Rais Samia kukutana na wawekezaji wakubwa watano sekta ya utalii,”amesema.

Alipoulizwa endapo kuna utafiti au uzoefu wa nchi nane zilizocheza filamu hiyo, Dk Abbasi amesema nchi hizo zimevutia watalii wengi licha ya kutoeleza kitakwimu.

Awali akieleza mafanikio ya ziara ya Marekani, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Zuhura Yunus ametaja zaidi ya manufaa 10 yanayohusisha mwelekeo mpya wa sekta ya biashara, uwekezaji, sekta ya kilimo na utalii.