Serikali ya Tanzania yakamilisha malipo ya ndege tatu
Muktasari:
- Serikali ya Tanzania imesema imekamilisha malipo ya ununuzi wa ndege mpya tatu, mbili zikiwa ni Airbus A220-300 na moja ni Dash 8-Q400De-Havilland.
Dodoma. Serikali ya Tanzania imesema imekamilisha malipo ya ununuzi wa ndege mpya tatu, mbili zikiwa ni Airbus A220-300 na moja ni Dash 8-Q400De-Havilland.
Hayo yamesema leo Jumanne Aprili 13, 2021 bungeni mjini Dodoma na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akiwasilisha bungeni mwelekezo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha za ofisi ya waziri mkuu na ofisi ya Bunge kwa mwaka 2021/22.
Amesema ndege hizo zinatarajiwa kuwasili kati ya mwaka 2021 au 2022 na hivyo kuwezesha Serikali kuwa na jumla ya ndege 12.
“Nitumie fursa hii kulipongeza Shirika la Ndege Tanzania kwa kuanzisha safari za kwenda Guangzhou, China,” amesema Majaliwa akibainisha kuwa safari hizo zitakuwa chachu ya kuimarisha biashara, utalii na ajira.