Serikali yaeleza mikakati kukabiliana upungufu mafuta ya kula

Serikali yaeleza mikakati kukabiliana upungufu mafuta ya kula

Muktasari:

  • Serikali imesema katika kukabiliana na upungufu wa mafuta ya kula nchini inatumia takribani  Sh470 bilioni kuagiza tani 360,000 za mafuta ya kula nje ya nchi kila mwaka.

Dodoma. Serikali imesema katika kukabiliana na upungufu wa mafuta ya kula nchini inatumia takribani  Sh470 bilioni kuagiza tani 360,000 za mafuta ya kula nje ya nchi kila mwaka.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema hayo leo Jumanne Aprili 13, 2021 bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha bungeni mwelekezo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha za ofisi ya waziri mkuu na ofisi ya Bunge kwa mwaka 2021/22.

Pia, amesema hivi karibuni  nchi  imekabiliwa  na  changamoto  ya uzalishaji  wa  ndani  wa  mafuta  ya  kutosha  ya  kula.

Majaliwa amesema hali hiyo imetokana na uzalishaji mdogo wa mazao ya  mbegu  ikiwemo nazi, alizeti,  pamba na  chikichi.

“Kwa  mfano, mahitaji  ya  mafuta ya kula kwa   mwaka   ni zaidi ya tani 570,000  wakati uzalishaji wa ndani ukikadiriwa kuwa tani 210,000,” amesema.

Amesema katika  kukabiliana  na changamoto  hiyo,  Serikali  inatekeleza  mikakati  ya kufufua  zao  la  chikichi ambalo  limeonekana  kuwa na  ufanisi  mkubwa  katika  uzalishaji  wa  mafuta  ya kula.

Majaliwa amesema mikakati hiyo   inakwenda   sambamba na kuimarisha  uzalishaji  kwenye mazao mengine  ya mbegu  ikiwemo alizeti,  nazi  na  pamba  ili  kupata mafuta  mengi na  kujitosheleza.