Serikali yafungua milango ya majadiliano kwa magazeti yaliyofungiwa

Serikali yafungua milango ya majadiliano kwa magazeti yaliyofungiwa

Muktasari:

  • Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa amesema agizo la Rais Samia Suluhu Hassan kutaka vyombo vya habari vilivyofungiwa kufunguliwa, linahusu televisheni za mtandaoni pekee.

Dar es Salaam. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa amesema agizo la Rais Samia Suluhu Hassan kutaka vyombo vya habari vilivyofungiwa kufunguliwa, linahusu televisheni za mtandaoni pekee.

Hata hivyo, Bashungwa ameeleza leo Jumatano, Aprili 7 2021 kuwa Serikali inafungua milango yake kwa vyombo vingine vya habari vilivyofungiwa kuangalia namna gani vinaweza kufunguliwa kwa mujibu wa sheria.

Kauli ya Bashungwa inatokana na madai ya wadau wa habari nchini, kutaka vyombo vya habari yakiwemo magazeti yaliyofungiwa kufunguliwa kupitia agizo hilo la Rais Samia.

Juzi, wakati akiwaapisha makatibu na manaibu makatibu wakuu wa wizara mbalimbali, Rais Samia aliagiza kufunguliwa kwa vyombo vya habari vilifungiwa na kwamba, vipewe uhuru katika kutekeleza majukumu yake bila kuvunja sheria.

“Nasikia kuna vyombo vya habari mlifungia, vifungulieni na vifuate sheria, tusiwape mdomo wa kusema kwamba tanaminya uhuru wa kuzungumza.

“Tusifungie kibabe, wafungulieni na kuhakikisha wanafuata sheria na miongozo ya Serikali. Hakikisheni kila mliyempa ruhusa ye kuendesha chombo cha habari afuate sheria.

Kanuni ziwe wazi kuwa kosa hili adhabu yake ni hii na mnakwenda kulingana na adhabu mlizoziweka kwenye kanuni, tusifungie kibabe, viacheni vifanye kazi,” alisema Rais Samia.

Baada ya kauli hiyo, wadau wa habari walipongeza uamuzi huo wa Rais Samia huku wakiomba agizo hilo lifanyiwe kazi mara moja na mamlaka husika.

Hata hivyo, mjadala mkali uliibuka baada ya Katibu Mkuu wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Hassan Abbasi kuhojiwa na kituo cha luninga cha Wasafi, akieleza kuwa uamuzi huo utahusu televisheni za mtandaoni pekee.

Baadhi ya wadau wa habari walitegemea kuona vyombo vyote vilivyofungiwa yakiwemo magazeti yakifunguliwa. Hata hivyo, kauli ya Bashungwa kuwa vyombo vingine nje ya televisheni za mtandaoni vinaweza kukaa mezani na wizara hiyo kila kimoja kulingana na kesi yake iliyosababisha kufungiwa.