Siha kuchanja watoto 27,000 polio, DC aonya
Muktasari:
- Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Peter Mahuu amesema malengo waliyopewa ni kuchanja watoto 27,000 wilayani humo, hivyo watakuwa wakichanja watoto 6,000 kwa siku.
Siha. Wakati Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro ikilenga kuwachanja watoto 27,000 chanjo ya ugonjwa wa polio, Mkuu wa Wilaya hiyo, Thomas Aposn, amesema hatasita kumchukulia hatua za kisheria mtu yeyote atakayekaidi agizo la kumpatia mtoto chanjo hiyo.
Akizungumza leo Mei 20 kwenye uzunduzi wa chanjo hiyo iliyofanyika kiwilaya katika Kijiji cha Matadi wilayani humo, Apson amewataka Wananchi kutoa ushirikiano ili uchanjaji ufanikiwe.
“Sasa kama Serikali tunatoa agizo maana yake siyo ombi, kwa sababu nia ya Rais wetu Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha jamii inakuwa na afya bora.
Amesema endapo mtoto asipochanjwa ndani ya miaka mitano anakuwa kwenye hatari ya kupata ulemavu wa viungo vya mwilini.
"Sisi tunamtazama mtu asiyetaka kuleta mtoto kwa ajili ya polio ni kama mhalifu, kwa sababu anakuwa na nia ya kuja kumfanya mwanaye kuwa mtu mwenye ulemavu na hivyo nguvu kazi ya Taifa itapungua," amesema Apson.
Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Peter Mahuu amesema malengo waliyopewa ni kuchanja watoto 27,000 wilayani humo, hivyo watakuwa wakichanja watoto 6,000 kwa siku.
Amesema kwa siku ya kwanza ya Mei 18 walivuka lengo kwa kuchanja watoto 6,950 akisema watavuka lengo ifikapo Mei 21.
Malawi ilitangaza mlipuko wa virusi vya polio mnamo Februari 17, 2022 baada ya mtoto mdogo kugundulika ambaye pia amekuwa mgonjwa kwanza Barani Afrika tangu kuthibitishwa kuwa hakuna virusi vya polio mwaka wa 2020.