TEF yamkaribisha Waziri Nape, yampa ujumbe

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye

Muktasari:

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limesema limepokea kwa matumaini uteuzi wa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye na linaamini kuwa Waziri huyo atasaidia kusukuma kwa kasi mchakato wa kuyafungulia magazeti yaliyofungiwa.

Dar es Salaam. Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limesema limepokea kwa matumaini uteuzi wa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye na linaamini kuwa Waziri huyo atasaidia kusukuma kwa kasi mchakato wa kuyafungulia magazeti yaliyofungiwa.

Taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile imesema kuwa Jukwaa hilo pia linamshukuru aliyekuwa waziri wa wizara hiyo, Dk Ashatu Kijaji ambaye ameteuliwa kuwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara.

Katika taarifa ya Balile amesema kuwa “Tunamkaribisha Mh Nape katika wizara hii na tunaamini atatusaidia kusukuma kwa kasi mchakato wa kuyafungulia magazeti tuliyoyataja, huku akiupa msukumo mpya mchakato wa kubadili sheria zinazosimamia taaluma ya habari kwa nia ya kukuza Uhuru wa Vyombo vya Habari nchini".

Balile amesema Jukwaa hilo linampongeza Dk Jim Yonaz kwa kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa wizara Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari  ambaye limesema limefanya naye kazi vizuri na kwa ukaribu katika mchakato wa kurekebisha Sheria za habari likisema linaamini mchakato huo unaendelea kuwa katika mikono salama.

“Tunampongeza Mohamed Hamis kwa kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari” imesema taarifa ya TEC huku ikimpongeza Dk Zainab Chaula, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo ambaye sasa ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu.

Jukwaa hilo limesema linaamini kuwa mawaziri walioteuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan kuunda upya Baraza la Mawaziri watakuza uhuru wa kupata habari, Uhuru wa Vyombo vya Habari na Uhuru wa Kutoa Mawazo, ambazo ni haki za msingi zinazowezesha haki nyingine kupatikana kwa mwanadamu.

Akizungumza na wanahabari muda mfupi baada ya kuapishwa leo Jumatatu Ikulu ya Chamwino Dodoma, Waziri Nape alisema anatambua kiu ya matarajio katika sekta hiyo aliyopewa inapotakiwa kwenda hivyo akiahidi kuyatendea haki matarajio hayo na kuomba ushirikiano.

“Ninachoweza kuahidi nitayatendea haki matarajio yote kuanzia ya Mungu, matarajio ya Rais, Serikali, chama changu, nchi yangu na matarajio ya dunia, niwaombe ushirikiano wenu tunajuana” alisema Waziri huyo ambaye ni mara yake ya pili kuwa kwenye baraza la mawaziri.

“Hili jambo ni la kwetu sote, ukipewa dhamana ya kuongoza sio kwamba unajua kila kitu ni vizuri tukashirikiana" alisema

Nape alishawahi kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Serikali ya awamu ya tano ambapo aliteuliwa na Rais John Magufuli Desemba 10, 2015 na uteuzi huo ulitenguliwa Machi 23, 2017.