Tetemeko lazua taharuki Dodoma

New Content Item (3)
New Content Item (3)

Muktasari:

  • Taasisi ya Jeolojia na Utafiti wa Madini (GST) imesema tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 5.5 katika katika kipimo cha richter limetokea mkoani Dodoma jana na kusababisha taharuki na sintofahamu.

Dodoma. Taasisi ya Jeolojia na Utafiti wa Madini (GST) imesema tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 5.5 katika kipimo cha richter limetokea mkoani Dodoma na kusababisha taharuki na sintofahamu kwa wakazi wa mkoa huo.

 Akizungumza leo Januari 18, 2022 Mjeolojia Mwandamizi wa taasisi hiyo Gabriel Mbogoni amesema tetemeko hilo lilitokea jana usiku.

Amesema kitovu chake kilikuwa Kaskazini Mashariki ya mji wa Dodoma kwenye safu za milima ya Chenene.

Amesema kitovu cha tetemeko ni umbali wa kilometa 44 kutoka Dodoma Mjini na lina ukubwa wa 5.5 katika kipimo cha richter.

“Hadi sasa hivi (mchana) hatujapata taarifa yoyote ya kutokea madhara zaidi ya taharuki na watu kuzusha sintofahamu kwa wakazi wa Dodoma,”amesema.

Amesema hadi kufikia leo mchana taarifa walizozipata za mahali ambako tetemeko hilo limeyakumba maeneo ya mkoa wa Dodoma hasa katika maeneo yanayozunguka mji wa Dodoma.

Amesema ukubwa wa tetemeko unaweza kusababisha nyufa katika majengo huku akibainisha kuwa madhara yanayoweza kusababishwa na ukubwa wa tetemeko yanategemea uimara wa majengo.

Mbogoni amesema Dodoma ipo katika ukanda wa bonde la ufa la Afrika Mashariki, eneo ambalo ni tete kwa matetemeko ya ardhi.