TRA: Bila TIN kosa la jinai kuanzia Januari

Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imesema hadi kufikia Desemba 31, mwaka huu kila mtu mzima nchini anatakiwa kuwa na Namba ya Mlipa Kodi (TIN).
Hayo yameelezwa na Ofisa Mkuu wa Usimamizi wa Kodi (TRA), Hamadi Mteri wakati wa ufunguzi wa semina kwa wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DCPC).

Alisema wa mujibu wa mabadiliko ya sheria, kila Mtanzania mwenye umri wa miaka 18 anapaswa kuwa na TIN ifikapo Desemba 31 mwaka huu, la sivyo litakuwa ni kosa kwa mujibu wa sheria.

Akifungua semina hiyo, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi (TRA), Richard Kayombo alisema Juni 30, tarehe ya mwisho wa mwaka fedha 2022/23 watakuwa wamekusanya Sh23.1 trilioni, mafanikio aliyosema yametokana na utoaji wa huduma za kidijitali na mifumo rafiki.

“Kwa sasa TRA imerahisisha mfumo kwa wafanyabiashara, hususani kwenye suala la namba ya utambulisho ya mlipa kodi (TIN), ulipaji wa kodi na mfumo wa forodha ambapo mteja anaweza kufanya vyote hivi kwa kurahisisha kazi zake," alisema Kayombo.