TTCL yatoa gawio la Sh2.1 bilioni kwa Serikali

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba

Muktasari:

  • Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limetoa gawio la Sh2.1 bilioni kwa Serikali ikiwa ni ongezeko la Sh600 milioni ukilinganisha na gawio la awali.

Dar es Salaam. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba amesema mwaka huu wanatoa gawio la Sh2.1 bilioni kwa Serikali kutokana na kukua kwa mapato ukilinganisha na mwaka uliopita.

Ameyasema hayo leo Jumanne ya Mei 21, 2019 katika hafla ya utoaji wa gawio kwa Serikali iliyoenda sambamba na uzinduzi wa awamu ya pili ya huduma ya video conference.

Kindamba amesema katika mwaka uliopita mapato yalikuwa Sh119 bilioni na mwaka huu imefikia Sh167 bilioni.

“Gawio hili ni ongezeko ya Sh600 milioni zaidi ya kile tulichokitoa mwaka jana na tunaahidi kuwa kadri huduma zetu zitakavyozidi kuimarika tutakuwa mstari wa mbele katika kutimiza wajibu wetu wa kisheria wa kuchangia pato la taifa.” Amesema Kindamba

Amesema katika kipindi cha mwaka mmoja wameweza kuboresha huduma kwa wateja kwa kufanya vituo vyao kuwa katika viwango vya kimataifa na wameongeza uwezo wa teknolojia na miundombinu kwa kampuni hiyo.

“TTCL imeendelea kuwa mwajiri mkuu katika sekta ya mawasiliano, tuna wafanyakazi takribani 1,500 nchi nzima lakini pia tumeanzisha utaratibu tukishirikiana na ofisi ya Waziri Mkuu juu ya kuwajengea vijana uwezo wa kuajirika vijana wanaotoka shule.” Ameongeza Kindamba

“Vijana hawa 200 kati yao tumewaajiri hapa na wengine wameajiriwa katika sehemu nyingine kwa sababu makampuni mengi yamekuwa yakitaka kuajiri walio na uzoefu sasa wataupata wapi hivyo tumeamua kuwasaidia.” Amesema.