Ushauri wa Juma Nature kwa Nandy na Zuchu

Muktasari:

Juma Nature amewashauri  wasanii wa Bongofleva wanaotamba kwa sasa, Nandy na Zuchu akiwataka kutobweteka na mafanikio waliyopata.

Dar es Salaam. Juma Nature amewashauri  wasanii wa Bongofleva wanaotamba kwa sasa, Nandy na Zuchu akiwataka kutobweteka na mafanikio waliyopata.

Amewataka watenge muda wa kukutana na watangulizi wao akiwemo msanii Lady Jay Dee.

Nature ambaye ni msanii wa muziki wa Bongofleva wa siku nyingi nchini Tanzania amewapa ushauri wawili hao wakati akizungumza na Mwananchi Digital lililotaka kusikia maoni yake baada ya wasanii hao kushinda tuzo za Afrimma.

Katika tuzo hizo Zuchu amshinda kipengele cha msanii bora anayechipukia huku  Nandy akishinda kipengele cha msanii bora wa kike Afrika Mashariki. Msanii Diamond Platnumz alishinda kipengele cha msanii bora wa kiume Afrika Mashariki.

Ushauri wa Juma Nature kwa Nandy na Zuchu

Akizungumzia ushindi wao, Nature amesema wana kipaji, “asikuambie mtu ukikubalika katika tuzo za kimataifa kama Afrimma wewe una kipaji na sio cha kukipuuza na kukubali kulewa sifa, ninachowasihi wadogo zangu Zuchu na Nandy wasichukulie poa hapo walipofikia wakaze buti.”

Aliwataka watambue kuwa mtaani wanapendwa na kukubalika kuliko wanavyofikiria na kusisitiza kuwa wanapaswa kutowasahau wala kuwadharau waliowatangulia.

“Watenge muda  wa kuwatafuta na kuchota mawili matatu kutoka kwa wakongwe wa muziki huo akiwemo Lady Jay Dee ambaye ni dada yao,” amesisitiza Nature.

Wakati Nature akitoa ushauri huo, Zuchu amewahi kumualika JJay Dee katika  uzinduzi wa EP yake uliofanyika Aprili, 2020 kwenye ukumbi wa Mlimani City.