Video: Simulizi aliyefumuliwa nyuzi na muuguzi

Simulizi ya mgonjwa aliyefumuliwa nyuzi na muuguzi

Muktasari:

  • Nilimwambia Mungu kitendo anachonifanyia dunia nzima itajua. Ndivyo alivyoanza kusema Zubeda Ngereza,  mwanamke aliyefumuliwa nyuzi alizoshonywa katika majeraha aliyoyapata baada ya kupata ajali ya pikipiki kwa sababu ya kushindwa kulipa  Sh10, 000 za matibabu.



Korogwe. Nilimwambia Mungu kitendo anachonifanyia dunia nzima itajua. Ndivyo alivyoanza kusema Zubeda Ngereza,  mwanamke aliyefumuliwa nyuzi alizoshonwa katika majeraha aliyoyapata baada ya kupata ajali ya pikipiki kwa sababu ya kushindwa kulipa  Sh10, 000 za matibabu.

Kitendo hicho kilifanywa na Dk Jackson Meli wa zahanati ya Kerenge mkoani Tanga na video zake kusambaa katika mitandao ya kijamii na kuzua sintofahamu huku mamlaka husika zikieleza kuwa tayari daktari huyo amechukuliwa hatua.

Akizungumza na Mwananchi Digital katika kijiji cha Kerenge Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga,  Zubeda  maarufu kama mama Barakati amesema tukio hilo lilitokea Julai 28, 2021.

Amesema siku hiyo akiwa katika usafiri wa bodaboda ilipata ajali na kuumia  usoni, mabegani na kwenye kiwiko na alifika kwenye zahanati hiyo kutibiwa majeraha aliyoyapata ikiwa ni pamoja na kushonwa.

Ameeleza kuwa baada ya kupatiwa matibabu,  Meli alianza kumdai  Sh10, 000 ya matibabu na yeye alimjibu kuwa atampatia, "nilimwambia fedha nitamlipa na nilianza kuwasiliana na watoto wangu."

"Baada ya kumjibu hivyo alibadilika na kusema nisimtanie ataniondoa dawa alizoniweka kwenye vidonda. Nikamjibu analetewa pesa lakini alisisitiza kuwa anahitaji pesa na malumbano yalipozidi alianza kunitoa pamba kwenye majeraha.

Alianza hadi kufumua nyuzi alizonishona nilisikia maumivu makali. Nilimwambia Mungu huyu mtu atalipa hili jambo,  nikasema ipo siku dunia nzima itajua alilonifanya. Hakujali alinijibu niende popote nikaseme."

Amesema baada ya sintofahamu hiyo watu waliingilia kati na baada ya muda akapata tena matibabu katika majeraha yake.