Wafanyabiashara nyamapori watakiwa kuwa na bustani kufuga wanyamapori
Askari wa Jeshi usu wakiwa kwenye gwaride wakati wa mahafali ya 58 ya chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka yaliyofanyika jana chuoni hapo ambapo jumla ya wanafunzi 356 walihitimu mafunzo mbalimbali ya Usimamizi wa wanyamapori.Picha na Janeth Joseph
Muktasari:
Serikali imewataka wafanyabiashara wenye mabucha ya nyamapori nchini kuanzisha bustani zao binafsi za kufuga kwa ajili ya kuchinja badala ya kutegemea wanyama ambao tayari wametunzwa na wako kwenye hifadhi za wanyamapori.
Moshi. Serikali imewataka wafanyabiashara wenye mabucha ya nyamapori nchini kuanzisha bustani zao binafsi za kufuga kwa ajili ya kuchinja badala ya kutegemea wanyama ambao tayari wametunzwa na wako kwenye hifadhi za wanyamapori.
Hayo yalisemwa jana na Naibu Katibu Mkuu wizara ya Maliasili na Utalii, Juma Mkomi wakati wa mahafali ya 58 ya chuo cha Usimamizi wa wanyamapori, Mweka ambapo jumla ya wanafunzi 356 walihitimu kozi mbalimbali za usimamizi wa wanyamapori.
Mkomi amesema bila kuwepo mashamba ya wanyamapori ya watu binafsi mabucha ya nyamapori nchini itakuwa ni ndoto ambayo haitekelezeki na kuwataka wadau na wenye nia ya kuanzisha mashamba na ranchi za wanyamapori kutumia nafasi hiyo ili kusaidia kuzalisha wanyama kwa wingi .
"Hivi karibuni kumekuwa na changamoto kubwa za bucha za wanyamapori, changamoto hii baada ya kutokea wakaja kulalamika kwetu kwamba mmetupa kauli tupu isiyokuwa na matendo, lakini kauli ile tuliyoitoa iliambatana na maelekezo kwamba tuwe na mashamba yetu ya wanyamapori alafu tuvune wale wanyama kutoka kwenye mashamba yetu tupeleke kwenye mabucha,"
"Sasa ukitaka sisi serikali tuvune wanyama wetu tukuletee kwenye bucha hilo haliwezekani, wataalam nendeni mitaani kaelimisheni kwamba mnahitaji kuwa na mabustani ya wanyamapori mkishastawisha mnavuna mnaenda kuuza kwenye mabucha ya watu wengine binafsi,"
Aliongeza kuwa "Sisi serikali hatuwezi kutunza, kuhifdhi alafu tukaanza kuuza tutagombana wenyewe kwa wenyewe,"
Pamoja na mambo mengine alikipongeza chuo hicho cha Usimamizi wa wanyamapori kwa kuweka mitaala mipya ya kuandaa wataalam na wadau wenye nia ya kuanzisha mashamba na ranchi za wanyamapori katika kuiendeleza sekta hiyo.
"Naahidi kuwa serikali na taasisi zake itaendelea kukiwezesha chuo pale itakapohitajika ili kuhakikisha kinafikia malengo haya yenye nia ya kufanikisha azma ya serikali, hapa nimetaja mashamba ya wanyamapori jamii ielewe kwamba bila kuwepo mashamba ya wanyamapori ya watu binafsi hata mabucha ya nyamapori itakuwa ndoto ambayo haitekelezeki,"
"Nimefarijika pamoja na kutoa mafunzo ya muda mrefu chuo kinaendesha mafunzo ya muda mfupi yanayoendana na mahitaji ya soko, niwapongeze kwa hatua hizi na kuwataka kuendela kubuni na kutangaza kozi nyingine za muda mfupi zitakazojibu changamoto mbalimbali za maendeleo ya uhifadhi na utalii
Mkuu wa Chuo hicho, Jafary Kideghesho alisema chuo hicho kimeendelea kutoa mafunzo bora na yenye tija na ya muda mfupi yanayoendana na mahitaji ya soko ambapo katika mwaka wa masomo 2022/23 kwa kurejea mitaala yake na kuandaa mingine mipya kuanzia ngazi za cheti hadi shahada za uzamili imeanza kutumika rasmi mwaka huu.
"Mitaala hii imezingatia mahitaji ya sasa ya soko na inalenga kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya uhifadhi wa wanyamapori na utalii ndani na nje ya nchi pamoja na kuwaandaa vijana waweze kujiajiri.
Pamoja na mambo mengine alisema chuo hicho kinaendelea na utafiti juu ya migongano kati ya wanyamapori hususani tembo na binadamu ili kubaini maeneo yanayoathiriwa zaidi na uvamizi wa tembo na kuja na mikakati ya kukabiliana na tatizo hilo ambalo limekuwa kilio kwa wananchi wengi.