Wakulima wagoma kuuza korosho wakilalamikia bei

Muktasari:

  • Wakulima wa korosho mkoani Lindi wamekataa kuuza korosho zao wakidai kuwa bei ya mnada kuwa chini

  


Lindi. Wakulima wa korosho mkoani Lindi wamegoma kuuza korosho zao wakidai kuwa bei ya mnada kuwa chini

Bei iliyotangazwa leo Jumamosi Oktoba 9, 2021 katika mnada  wa kwanza ulioendeshwa na Chama  Kikuu cha Ushirika cha Lindi (Mwambao) katika Kijiji na Kata ya Nachunyu ulikuwa na bei ya kati ya Sh2,275 na Sh2,010.

Mmoja wa wakulima hao, Ali Mohamed amesema wamekataa kuuza kwa sababu bei ni ndogo kulinganisha na gharama za uzalishaji.

"Sisi hatutaki kuuza korosho kwa bei hiyo, angalau bei ingekua Sh3,000. Korosho zina gharama kubwa kuziandaa, kuna makato mengi, Serikali, waokotaji wote wanatakiwa kulipwa, halafu bado pembejeo," amesema Ally.

Akizungumza katika mnada huo Mkuu wa wilaya ya Lindi, Shaibu Ndemanga amesema utaitishwa mnada mwingine Jumamosi Oktoba 16, 2021.

“Utaratibu ni kwamba kwa kuwa hatujakubaliana na bei na kwa kuwa tumeamua wote kwa umoja wetu tutulie utaratibu ni kwamba jumamosi  tutaingiza tena korosho zetu sokoni," Ndemanga baada ya mgomo wa wakulima.

Wakulima waliokusanyika mnadani hapo wameiomba Serikali iwasaidie kuongea na wanunuzi ili bei ipande