Wakulima wapata hofu wadudu kuvamia mazao

Wakulima wapata hofu wadudu kuvamia mazao

Muktasari:

  • Wakulima na wakazi wa Wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha wamekumbwa na hofu baada ya kuonekana wadudu wanaodaiwa kuwa ni nzige katika makazi yao.

Arusha. Wakulima na wakazi wa Wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha wamekumbwa na hofu baada ya kuonekana wadudu wanaodaiwa kuwa ni nzige katika makazi yao.

Wadudu hao wanaodaiwa kushambulia mazao walianza kuonekana maeneo ya Namanga mpakani mwa Kenya na Tanzania na baadaye kuingia nchini.

Mkuu wa wilaya ya Longido, Frank Mwaisumbe amesema nzige hao wamesambaa sehemu kubwa ya Wilaya hiyo.

"Walianza kuonekana maeneo ya mpakani na mji wa Namanga na baadaye nimepata  taarifa kuoneka na maeneo mengine," amesema.

Amebainisha kuwa tayari amewasiliana na viongozi wa Mkoa na Wizara ya Kilimo walioahidi kutuma wataalam haraka iwezekanavyo.

"Naomba niwaondoe hofu wananchi kwani Serikali inashughulikia tatizo hili kwa wakati," amesema.

Mkazi wa Longido, Jeremiah Sanka amesema wamekumbwa na hofu ya mazao kuliwa na nzige, “wametuma wengi kwenye mashamba na muda huu ndio mahindi yameanza kuota  kama yakiliwa ni hasara  kubwa.”