Wauguzi kujikita magonjwa yasiyoambukiza

Muktasari:

Chama cha Wauguzi tawi la Hospitali ya Taifa Muhimbili kimejipanga kuweka nguvu ya elimu dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza, ikiwa ni mwendelezo wa maadhimisho ya siku ya wauguzi duniani.

Dar es Salaam. Katika mwendelezo wa maadhimisho ya siku wauguzi duniani inayofanyika Mei 12, Chama cha Wauguzi tawi la Hospitali ya Taifa Muhimbili kimejipanga kuweka nguvu ya elimu dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

Mkakati huo umekuja kufuatia kile kinachoonekana kuongezeka kwa idadi ya watu wenye magonjwa hayo na wanafika hospitali kwa kuchelewa.

Mwenyekiti wa chama cha wauguzi Taasisi ya Mifupa (MOI), Moses Moses mwenendo wa wagonjwa wanaokwenda hospitali wakiwa katika hatua za mwisho umekuwa ukiongeza hivyo wameona kuna haja ya wao kuingia kwenye jamii.

“Tunaadhimisha siku ya wauguzi katika taasisi zote zilizo ndani ya Muhimbili tumeona tusiishie kusherehekea ila tutumie taaluma zetu kuisaidia jamii, kuna haja kubwa ya elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza na lishe.

 “Hilo tutalifanya Mei 26 katika viwanja vya Mwembe yanga, pamoja na kutoa elimu pia tutatoa nafasi ya watu kupimwa bure wajue kuhusu afya zao. Kuna changamoto ya watu kutojua hali zao matokeo yake wanafika kwenye matibabu kwa kuchelewa,” amesema Moses.

Pamoja na kupima afya na kutoa elimu, siku hiyo pia watachangia damu na kukusanya damu kwa watu wengine watakaojitokeza kuchangia.

“Tuwakumbushe watanzania wenzetu kuwa hizi taasisi zote zinahitaji damu, hakuna mahali tunaweza kununua damu hivyo ni wajibu wetu kama binadamu kujitolea ili tuweze kuokoa maisha ya wengine.”

Kwa upande wake mwenyekiti wa Tana MHN, David Mpagika amesema maadhimisho hayo yatahusisha pia kongamano la kisayansi ambalo litafanyika Mei 27.

“Kutokana na majukumu yetu, kuna tafiti mbalimbali za kisayansi ambazo zimefanywa na wauguzi zitawasilishwa siku hiyo lengo likiwa kushirikishana na kufundishana namna ya kukabiliana na changamoto wakati wa utoaji huduma.

“Kwa kifupi maadhimisho yetu yataanza Mei 25 hadi 27, katika siku hizo wauguzi watafanya mambo mbalimbali ikiwa ni sehemu ya mchango wao kwenye jamii wanayoihudumia kila siku,” amesema.