Wawakimbia wenza wao kliniki kisa kupima VVU

Muktasari:

  • Wanaume mkoani Shinyanga wanawakimbia wake zao kwenda nao kliniki, kisa wanaogopa kupima VVU

Shinyanga. Baadhi ya wajawazito mkoani Shinyanga wamekuwa wakifanyiwa ukatili na wenza wao pale wanapowataka kwenda nao kliniki kupima  maambukizi ya Ukimwi.

 Hayo yamesemwa na mganga mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt Yudas Ndungile kwenye maadhimisho ya siku  ya Ukimwi duniani yaliyofanyika katika mji mdogo  wa Isaka halmashauri ya Msalala  ambapo alisema kuwa wanaume nao wanapaswa kuongoza  na wenza wao pasipo shaka kwenda kupima Ukimwi.

Dkt Ndungile amesema kuwa kiwango cha maambukizi ya virusi  vya Ukimwi Mkoa wa Shinyanga kiko juu kwa asilimia 5.9 ukilinganisha na kiwango cha kitaifa 4.7

"Wanaume wapendeni wenza wenu wanapopata ujauzito muwasindikize kliniki mkapime afya kwa pamoja  msiwaache pekee yao wakapime  mshuhudie wote na kupewa ushauri nasaha wa namna ya kuishi"amesema dkt Ndungile.

Dkt Ndungile amesema kuwa maambukizi ya virusi vya ukimwi  yameongezeka  kutoka asilimia 3.9 mwaka jana  hadi kufikia asilimia 4.7  mwaka huu huku watu zaidi ya 6000 wamebainika kuwa na maambukizi mapya.

Ofisa maendeleo ya jamii mkoa wa Shinyanga Tedson Ngwale amesema  kuwa  siku hizi wajawazito nao wamekuwa na mtindo wa kuchukua mwanaume yoyote ambaye siye mume wake nakwenda naye kliniki  Ili mradi akapate huduma ikiwemo kupima ukimwi jambo ambapo ni hatari.

Kaimu meneja wa Shirika la Uheso linalojishughulisha na jamii inayoishi na virusi vya Ukimwi wilayani Kahama  David Edson amesema kuwa wamekuwa wakihamasisha kundi la vijana  wasichana katika suala la kupima VVU  na kuwapa ushauri nasaha.

Scholastika Kapera mwenyekiti wa  mtandao wa watu wanaoishi na virusi vya ukimwi  (WAVIU) amésema  kumekuwa na malalamiko kwa wajawazito wanapokwenda kliniki wanaelezwa kwenda na wenza lakini wanaume wamekuwa hawapo tayari , badala yake  yake wamekuwa wakikodi wanaume kuwasindikiza kliniki na ndio hao wanaopimwa virusi vya Ukimwi.