Wawili Chadema watimkia CCM

Mwanachama wa Chadema mkoani Singida, Philemon Ghula aliyehamia CCM

Muktasari:

  • Wanachama wawili wa Chadema wamehama chama hicho na kujiunga na CCM, kwa madai kukosekana kwa demokrasia halisi wanayoinadi viongozi wao kila siku.

Singida. Wanachama wawili wa Chadema wamehama chama hicho na kujiunga na CCM, kwa madai kukosekana kwa demokrasia halisi wanayoinadi viongozi wao kila siku.


Wanachama hao ni aliyekuwa kampeni meneja wa Kata ya Unyahati, Philemon Ghula na aliyekuwa mgombea udiwani Kata ya Makiungu, Julius Sunna.


Akizungumza mara baada ya uamuzi huo Ghula amesema wamechukua uamuzi huo ili kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan.


"Rais Samia anafanya kazi nzuri sana inayoonekana na kila mmoja wetu hivyo tuna kila sababu ya kumuunga mkono," amesema Ghula.


Kwa upande wake Sunna amesema amechukua uamuzi huo kutokana na kuchoshwa na ubabaishaji wa viongozi wao wasiotaka maendeleo ya wananchi.


"Sisi tumetumikia Chadema kwa miaka mingi tena kwa kujitolea, lakini hawakutambua thamani na mchango wetu," amesema Sunna.

Mwanachama wa Chadema Singida, Julius Sunna  aliyehamia CCM


Kwa upande Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ikungi, Mika Likapakapa amewapongeza wanachama hao wapya na kuwakaribisha wakijenge chama na nchi ili kuchochea maendeleo ya wananchi.