Wawili wafariki kwa kukanyagwa na treni Moshi
Muktasari:
- Watu wawili wamefariki duniani papo hapo wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro baada ya kugonga treni iliyokuwa ikitokea Jijini Arusha kuelekea Jijini Dar es salam.
Moshi. Watu wawili wamefariki dunia papo hapo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro baada ya kugonga treni iliyokuwa ikitokea jijini Arusha kuelekea jijini Dar es salam.
Tukio la kwanza limetokea saa 12 asubuhi katika eneo la Mabogini, Kata ya Bomambuzi na tukio la pili saa tano asubuhi katika eneo la Stesheni Kata ya Kahe, Wilaya ya Moshi.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Simon Maigwa amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo ambapo amesema miili ya watu hao imehifadhiwa katika hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Mawenzi.
Kamanda Maigwa amewataja waliofariki kuwa ni Salim Abuu (25) mkazi wa Kata ya Bomambuzi ambaye alikuwa akivuka reli akiwa amelewa bila kuwa na tahadhari na wa pili amemtaja ni mzee wa umri kati ya miaka kati ya 75 hadi 80 mkazi wa Kahe ambaye bado hajafahamika jina na kwamba alikuwa na tatizo la kutokusikia alishindwa kusikia honi wakati wa mngurumo wa treni.
"Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linaendelea kusisitiza kwa wananchi waache tabia ya kutembea barabara ya treni bila kuchukua tahadhari, kufanya hivyo kunasababisha vifo vinavyoweza kuepukika na Serikali kupoteza nguvu kazi ya Taifa letu," amesema Kamanda Maigwa.