Wazee ACT-Wazalendo wataka wazee kujiandaa kuhesabiwa

Muktasari:

Sensa ya Watu na Makazi nchini Tanzania itafanyika Agosti 23, 2022 huku wito ukitolewa kwa wananchi mbalimbali kujiandaa kuhesabiwa

Dar es Salaam. Zikiwa zimebaki siku 17 kabla ya Sensa ya Watu na Makazi, Ngome ya Wazee ACT Wazalendo inawakumbusha wazee wote nchi nzima bila kujali itikadi zao za kisiasa, kujitokeza kwa wingi siku hiyo kuhesabiwa.

 Sensa ya Watu na Makazi itafanyika Agosti 23, 2022 Nchini kote.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi Agost 6, 2022 Mwenyekiti wa Ngome ya Wazee ACT-Wazalendo, Yasin Mohamed Gumsan amesema kama wazee wameona wanahitaji mambo mengi ambayo Serikali haina budi kuyateekeleza.

"Bila kuhesabiwa Serikali haitaweza kutusaidia kwa kuwa itakuwa haijui idadi yetu halisi nchi nzima,” amesema

“Chama chetu ambacho kinajiendesha kisayansi, kinahitaji zaidi kutumia taarifa za utafiti na takwimu ili pamoja na mambo mengine kujiwekea malengo ya Kisiasa," amesema Gumsan.

Gumsan amesema bila kujulikana kwa idadi kamili nchi nzima, hawawezi kuhudumiwa hivyo itawapasa kusubiri tena kwa kipindi cha miaka kumi ijayo na kuwataka wazee kutopoteza fursa hiyo, na badala yake wajitokeze bila kukosa.

"Sisi Wazee wa ACT Wazalendo tunaleta kilio cha wazee wenzetu nchi nzima kwa Rais Samia Suluhu Hassaan, kwa lengo la kukutana na wazee kwa lengo la kusikia kilio chetu, kwa kuwa wazee siku zote watabaki kuwa nguzo muhimu yenye maarifa, ufundi na hekima," amesema.