Waziri mkuu aigiza TRA kujenga mahusiano mazuri na wawekezaji

Muktasari:

  • Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kujenga mahusiano mazuri na wawekezaji ili waweze kufanya vizuri katika uzalishaji na kuchangia pato la Taifa.


Rungwe. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kujenga mahusiano mazuri na wawekezaji ili waweze kufanya vizuri katika uzalishaji na kuchangia pato la Taifa.

Waziri mkuu ametoa maagizo hayo leo Jumamosi Novemba 27, 2021 alipofanya ziara ya kikazi ya kukagua mradi wa kiwanda cha kuzalisha maji ya kunywa cha Tukuyu Springs Water kilichopo Wilayani Rungwe mkoani Mbeya.

Majaliwa amesema kuwa Serikali inatambua mchango mkubwa wa wawekezaji, Mamlaka hiyo ya Mapato ijenge mazingira mazuri kwa mustakabali wa Taifa ikiwa ni kutekeleza agizo la Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake, Meneja Mradi wa Kampuni ya Tukuyu Springs Waters, James Mgeni amesema licha ya uzalishaji kuwa mkubwa, changamoto ni ubovu wa miundombinu ya barabara kutokuwa rafiki hususan katika kipindi cha mvua.

''Mheshimiwa Waziri Mkuu soko la maji ni kubwa lakini kuna changamoto kubwa ya miundombinu  kwani wastani kwa siku tunazalisha chupa 36,000 za maji na kusambazwa maeneo mbalimbali nchini,”amesema Meneja huyo.