Waziri Mkuu amsimamisha kazi Afisa Mipango Liwale

Waziri Mkuu amsimamisha kazi Afisa Mipango Liwale

Muktasari:

  • Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amemsimamisha kazi Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale, Omary Chingwile ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za matumizi mabaya ya fedha za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Liwale.


  

Liwale. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amemsimamisha kazi Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale, Omary Chingwile ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za matumizi mabaya ya fedha za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya hiyo.

Majaliwa ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi juu ya tuhuma hizo.

Waziri Mkuu amemsimamisha kazi mtumishi huyo jana Alhamisi Oktoba 7, 2021 wakati akizungumza na madiwani, watumishi na wananchi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo  akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Lindi.

“Hatuwezi kufanya mchezo na fedha ya Serikali. Tunahitaji kila mradi uende vizuri, fedha iliyoletwa lazima itumike kama ilivyokusudiwa.” Amesema Majaliwa.

Pia, Waziri Mkuu amelitaka Balaza la madiwani wa Halmashauri hiyo  lisimamie fedha za miradi zinazotolewa katika Halmashauri  ikiwa ni pamoja na kubuni vyanzo vipya vya mapato.

“Madiwani Halmashauri yenu inakusanya mapato hadi asilimia 100 lakini hatujawahi kuona mradi wowote unaotekelezwa na halmashauri na ukawa wa mfano.” Majaliwa.

Amesema Halmashauri hiyo imekuwa ikiweka makadirio madogo ya makusanyo ili ionekane inakusanya kwa asilimia kubwa lakini mapato hayakusanywi kwa njia ya mtandao.

Amemuagiza Mweka Hazina wa Halmashauri hiyo, Gervas Bidogo kuhakikisha vifaa vyote vya kukusanya fedha kwa njia ya mtandao vinafanya kazi.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Liwale, Judith Nguli kufuatilia fedha za wakulima wa korosho na ufuta ambao hawajalipwa na vyama vya ushirika abavyo vilikusanya mazao yao.

“Nakupongeza Mkuu wa Wilaya kwa kuchukua hatua ya kumsimamisha kazi Afisa Ushirika, Ephraim Kipomela kutokana na upotevu wa fedha za ushirika usiishie hapo hakikisha vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama vinafanya uchunguzi na kubaini namna fedha hizo zilivyopotea.” Majaliwa.