Mazoezi yamfaayo mtoto mchanga, faida zake

Mtoa huduma za afya akimuelekeza mama mjamzito namna ya kutumia simu ya mkononi wakati wa dharura Picha na Maktaba.
Muktasari:
- Mazoezi kwa watoto wachanga yanawasaidia kunyoosha viungo vyao na kuvifanya kuwa imara zaidi wanapokua.
Ni kazi ngumu kumlea mtoto tangu anapozaliwa hadi kupevuka.
Hata hivyo, malezi bora kwa watoto wachanga ni mkusanyiko wa mambo mengi yakiwemo lishe bora, malazi mavazi na tiba na kinga ya maradhi.
Miongoni mwa mambo ya kuzingatia katila malezi ya mtoto ni kumkinga na maradhi sambamba na kuuweka mwili wake katika mazingira mazuri
Kama ilivyo muhimu kufanya mazoezi kwa watoto wakubwa na watu wazima, watoto wachanga vile vile wanao umuhimu wa kufanyishwa mazoezi.
Hivyo basi, mazoezi kwa mtoto mchanga ni miongoni mwa mambo muhimu ya kuzingatia kwa wazazi au hata walezi wanaopewa jukumu hilo.
Jambo la muhimu la kuzingatia kwa mzazi au mlezi ni kuwa tayari kujifunza kila siku mbinu mpya zitakazosaidia kuboresha na kufanikisha malezi stahiki ya mtoto mchanga hadi anapoondokana na uchanga wake.
Vile vile, mzazi au mlezi hana budi kufahamu kuwa kwa jinsi siku zinavyopita, na kwa kadri mtoto anavyokua, mambo mbalimbali hujitokeza kwa mtoto hali inayopaswa kuendana na kasi ya kujifunza kila siku ili kuelekea mafanikio.
Kwa kawaida ukiwa mama unapaswa kujifunza mambo mengi kuhusu watoto kila kukicha na unapaswa pia kuhakikisha kile kitu ulichojifunza unakifanyia kazi ili kumpa kichanga makuzi yanayostahili.
Tofauti inayopatikana hapa ni kuwa wakati makundi hayo mengine hufanya mazoezi kwa kutumia nguvu zao, watoto wachanga hupaswa kufanyishwa mazoezi na wazazi na walezi wao.
Mazoezi haya ya mtoto mchanga yanafanyika kwa utaratibu wa massage ambapo kinachofanyika ni kumkanda au kumfanyia masaji sehemu mbalimbali za mwili wake.
Watoto wanaposuguliwa taratibu tumboni hii huweza kuwafanya wajisikie vizuri kwa vile huhisi kwamba angalau mzazi ama mlezi anajitahidi katika kufanya kitu fulani kusaidia kumwondolea shida.
Jinsi ya kufanya
Ikumbukwe kuwa viungo vya mtoto mchanga ni laini, unapomfanyisha mazoezi mtoto mchanga unapaswa kuepuka kutumia nguvu na badala yake kuhakikisha unatulia na kufanya hivyo kwa uangalifu.
Masaji yenyewe iwe ni ile ya kumsugua taratibu mgongoni, kumnyoosha viungo vya mwili wake hususani sehemu za miguu, mikono pamoja na vidole.
Masaji hii inawekwa kufanywa kwa kutumia mafuta laini ya mtoto, mafuta ya nazi yaliyotengenezwa na mama mwenyewe ni mazuri kwa kuwa hayana kemikali.
Imeandaliwa na Joyce Mmasi, kwa msaada wa mtandao