Pablo apewa siku 7 Simba

Pablo awazuga Wasauzi

KOCHA Mkuu wa Simba, Pablo Franco amepewa wiki moja kuandaa ripoti maalumu kwa ajili ya masuala ya kiufundi kabla ya msimu ujao kuanza mambo gani anayotaka yafanyike kufanya vizuri.

Habari za uhakika kutoka ndani ya Simba zinasema kwamba viongozi wamemwambia Kocha huyo awape kila kitu anachokifikiria lakini pia awaweke wazi nini hatma yake. Simba imepania kucheza nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao unaoanza mwishoni mwa mwaka huu.

Viongozi hao wameliambia Mwanaspoti kwamba wamezisikia taarifa za kocha wao kuhitajika na Orlando Pirates ya Afrika Kusini ingawa wamedai kuwa kocha hajawapa taarifa rasmi.

“Sisi tumemwambia atupe ripoti ambayo itaendana na matakwa yake na kama pia hatakuwepo atuandae mapema ili tujue tunaandaaje timu, kwasababu hatuwezi kuandaa timu kwa programu yake halafu anakuja kocha mwingine ambaye ni vitu viwili tofauti,” alidokeza kiongozi mmoja wa Simba.

Hata hivyo, Pablo alisema hawezi kuitolea ufafanuzi taarifa isiyokuwa rasmi hasa kuhusu hatma yake ya msimu ujao.

“Muda sahihi wa kujibu suala hilo utakapofika nitakujulisha, ila nafahamu ligi ya Afrika Kusini ni kubwa na nzuri,” alisema Pablo akizungumzia suala hilo.