Samatta aibadili Stars

Muktasari:

Kocha wa Taifa Stars, Etienne Ndayiragije amesema licha ya kumkosa nahodha wake, Mbwana Samatta, ambaye ni majeruhi, lakini ana imani na wachezaji waliopo kuwa wataipa ushindi timu hiyo kesho.

Dar es Salaam. Kocha wa Taifa Stars, Etienne Ndayiragije amesema licha ya kumkosa nahodha wake, Mbwana Samatta, ambaye ni majeruhi, lakini ana imani na wachezaji waliopo kuwa wataipa ushindi timu hiyo kesho.

Ni rasmi sasa majukumu ya ufungaji yatakuwa chini ya mshambuliaji wa Simba, John Bocco akisaidiana na Simon Msuva, Ditram Nchimbi, Idd Nado, Thomas Ulimwengu na Adam Adam.

Ndayiragije alisema wapo pamoja na Samatta na anaamini ushindi katika mchezo huo utakuwa ni faraja kwa nahodha huyo kumtakia kupona haraka.

Taifa Stars iliyo Kundi J la mashindano ya kufuzu kwa fainali za Mataifa Afrika (Afcon) itaikabili Tunisia kesho kwenye Uwanja wa Olympique de Rades mjini Tunis na timu hizo zitarudiana Novemba 17 jijini Dar es Salaam.

Ndayiragije alisema wanasikitika kumkosa Samatta katika mechi zote mbili kutokana na kuwa majeruhi, lakini hana hofu kwani wachezaji waliopo katika kikosi hicho wana morali kuelekea mchezo huo.

“Maandalizi yetu yalikuwa mazuri katika kambi yetu ya siku chache hapa Uturuki na leo (jana) tunaelekea Tunisia tayari kwa ajili ya mchezo huo.

“Tumefanya mazoezi vizuri na hakuna mchezaji aliyeumia, wote wapo vizuri wana hamu ya kufanya kitu ambacho tunahitaji kufanya. Ushindi utatuweka nafasi nzuri zaidi katika msimamo na tutakuwa na furaha kwa ajili ya hilo kwa sasa,” alisema Ndayiragije.