Kakolanya kusalia Simba

VINARA wa Ligi Kuu Bara, Simba wanaendelea kuimarisha kikosi chao kwa kuwaongeza mikataba wachezaji ambao mwisho wa msimu huu unamalizika.

Mmoja wa watu waliokuwa katika  benchi la Simba, ameliambia Mwanaspoti kuwa wapo katika mchakato wa kuongeza mikataba wale wachezaji ambao mwisho wa msimu huu inamalizika akiwepo kipa, Benno Kakolanya.

Alisema mchana wa leo Juni 7, wanaweza kumalizana na kipa wao namba mbili,  Kakolanya katika suala la kumuongeza mkataba mpya kwani ule wa awali unamalizika mwisho wa msimu huu.

"Awali Kakolanya aliniambia tayari wameshamalizana na uongozi katika mazungumzo ya mkataba mpya ingawa kulikuwa na kuvutana kila mmoja kwa upande wake ila walikubaliana," alisema mtoa taarifa huyo na kuongezea;

"Tuliwasiliana na kunieleza kuwa mchana wa leo Juni 7, atakwenda ofisini kusaini mkataba mpya wa miaka miwili kama ulivyokuwa ule wa awali."

Simba walimsajili Kakolanya kutokea Yanga 2019-20, kwa mkataba wa miaka miwili ambao mwisho wa msimu huu ulikuwa unamalizika.

Katika hatua nyingine kikosi cha Simba baada ya mapumziko ya siku moja kesho Juni 8, 2021 watarejea kambini kwa ajili ya kuanza mazoezi na mchezo unaofuata.

Mazoezi hayo watafanya wale wachezaji ambao hawapo katika majukumu ya timu za taifa na yatasimamiwa na kocha wa viungo, Adel Zrane kwani wataanzia gym kwanza.