Mayele afunguka ishu ya bao moja Yanga

Muktasari:

  • MSHAMBULIAJI wa Yanga, Fiston Mayele ni kama amesikia malalamiko ya mashabiki wa timu hiyo ambayo imekuwa na mwendelezo wa kupachika bao moja moja tangu imeanza msimu na kufichua siri mbili zilizoko nyuma ya hilo.

MSHAMBULIAJI wa Yanga, Fiston Mayele ni kama amesikia malalamiko ya mashabiki wa timu hiyo ambayo imekuwa na mwendelezo wa kupachika bao moja moja tangu imeanza msimu na kufichua siri mbili zilizoko nyuma ya hilo.

Yanga imecheza michezo miwili ya ligi kwa kuanza na Kagera Sugar ugenini na kuambulia ushindi wa bao 1-0 likifungwa na Feisal Salum, mchezo wa pili ulikuwa kwa Mkapa dhidi ya Geita Gold ambapo iliibuka na ushindi wa bao 1-0 likifungwa na Jesus Moloko.

Mayele ndiye mfungaji wa bao pekee kwenye mchezo wa kirafiki dhidi ya JKU juzi usiku kwenye Uwanja wa Mkapa Dar es Salaam aliliambia mwanaspoti kuwa: “Tupo vizuri eneo la ushambuliaji na tupo wachezaji wengi na wote tunauwezo shida zilizopo ni kutokuzoeana sambamba na kila mchezaji kutaka kufunga hili ni tatizo dogo na linaweza kupatiwa ufumbuzi tunaomba muda.”

“Ni mapema sana kulaumiwa ukizingatia tunapata bao moja na ni la ushindi hatujaruhusu kufungwa na katika bao hilo moja kunakuwa na nafasi nyingi zinazotengenezwa hivyo hii ni moja ya sifa kwetu kwamba tuna uwezo mkubwa tukitulia,” alisema.

Mayele alisema anatamani kufunga kwenye kila mchezo kwasababu ndio kazi iliyomleta Yanga na anatarajia kufanya makubwa zaidi ndani ya timu hiyo ambayo ameimwagia sifa kuwa ina nyota wengi wenye uchu wa mafanikio na malengo yao kama timu ni kufanya vizuri kwenye kila mchezo.

Shabiki wa Yanga, Tumbe Makame alisema wachezaji wote waliowasajili wana viwango na kwamba hakuna hata mmoja wa kuokoteza katika kikosi chao msimu huu.