Pablo mbinu 3 tu zinatosha Simba

Muktasari:

  • KOCHA wa Simba, Pablo Franco ameliambia Mwanaspoti kwamba kwa aina ya wachezaji aliowakuta Msimbazi mbinu tatu tu zinatosha kumpa mafanikio msimu huu.

KOCHA wa Simba, Pablo Franco ameliambia Mwanaspoti kwamba kwa aina ya wachezaji aliowakuta Msimbazi mbinu tatu tu zinatosha kumpa mafanikio msimu huu.

Amekiri kukutana na wachezaji wenye ubora na wanaofiti kwenye mifumo yake mitatu ambayo anaamini inaweza kuwa chachu ya mafanikio yake ndani ya klabu hiyo kwa muda mfupi.

Alisema tangu ameanza kufundisha soka amekuwa akiamini katika umiliki wa mpira kucheza soka la pasi nyingi baada ya kukaa na timu yake kwa muda na kufanikiwa kupata ushindi wa kwanza anaamini mifumo yake pendwa itachukua nafasi kubwa.

Alisema kwenye timu yake atakuwa akifundisha falsafa ya kumiliki mpira, kucheza soka la chini na kushambulia kwa haraka atakwenda na 4-1-4-1, 4-2-3-1 na 4-4-2 Diamond.

“Kocha yoyote duniani huwa na falsafa zake ndani yake zinazaa mifumo bora ili kwenda kuwazidi wapinzani katika kile mechi ambayo watakuwa wanacheza,” alisema Kocha huyo ambaye mwezi ujao anakabiliwa na Dabi ambayo amesema anaichukulia kawaida.

“Nimeanza kulifanyia kazi hilo ndani ya muda mfupi niliokuwa katika kikosi cha Simba na matunda kwa uchache yameanza kuonekana katika mechi na Ruvu Shooting kwani mbali ya ushindi walicheza soka la kuvutia tofauti na mechi tano zilizopita,”

“Ukiangalia mechi na Ruvu tulimiliki mpira zaidi, tulishambulia kwa aina tatu tofauti, tulicheza mifumo miwili 4-2-3-1 ambao tulianza nao na baadae tulikuja kumalizia na 4-4-2, Diamond,” alisema.

Mifumo hiyo mitatu ambayo Franco anapenda kutumia ukianza na 4-1-4-1 maana yake wanakuwa na mabeki wanne, kiungo mmoja mkabaji, viungo wanne washambuliaji na straika mmoja.

Kwenye 4-1-4-1, atakuwa na uhakika kwenye ulinzi mbali ya uwepo wa mabeki wanne kutakuwa na mchezaji mmoja juu yao kiungo mkabaji, atamiliki mpira zaidi eneo la kiungo na kuzalisha mabao hapo kupitia Kibu Denis, Rally Bwalya na Hassan Dilunga.

Wakati mfumo 4-4-2 Diamond, ambao aliutumia kipindi cha pili dhidi ya Ruvu maana yake atakuwa na mabeki wanne, viungo watano na washambuliaji wawili asilia.

Tafsiri yake ni kwamba atakuwa na uhakika katika ulinzi, uwepo na idadi kubwa ya wacheza si chini ya wanne katika eneo la kiungo kama, Jonas Mkude, Mzamiru Yassin, Dilunga na Bwalya muda huo huo watafanya mashambulizi ya haraka kwa sababu wataanza na mastraika wawili asilia.

Pablo alisema mfumo wa 4-2-3-1, ambao anapenda kutumia na alianza nao katika mechi na Ruvu hautakuwa shida kwake kwani ndani ya misimu mitatu umekuwa ukitumika ndani ya kikosi.

Alisema mfumo huo unaanza na mabeki wanne, viungo wawili wakabaji, viungo watatu washambuliaji na straika mmoja atakuwa na uwezo wa kulinda na kuzuia mashambulizi ya timu pinzani.

“Mfumo huu katika kipindi cha kwanza ulitulipa kwa kupata mabao mawili kutoka kwa straika Meddie Kagere na lingine moja kutoka kwa Kibu ambaye alicheza eneo la kiungo,” alisema