Rais wa FIFA kutua Arusha leo

Arusha. Rais wa Shirikisho la Soka la Duniani (FIFA), Gianni Infantino anatarajia kuwasili leo saa 2 usiku jijini Arusha, kwa ajili ya kushiriki mkutano mkuu wa 44 wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) huku tayari zaidi ya wageni 500 wakiwa tayari Arusha.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mohamed Mchengerwa ametoa taarifa hiyo, leo Agosti 9, 2022 katika mkutano na waandishi wa habari  katika kituo cha mikutano cha Arusha, (AICC) kuelezea maandalizi ya mkutano wa CAF ambao unafanyika kesho jijini Arusha.

Waziri Mchengerwa amesema sambamba na Rais wa FIFA, pia Rais wa  Shirikisho la Soka nchini Qatar (QFA) Sheikh  Hamad Bin Khalifa atashiriki sambamba na marais wa vyama vya soka kutoka katika mataifa 52 barani Afrika na wajumbe wa mkutano mkuu wa CAF.

"Kutakuwa na wageni zaidi ya 500, kutoka Afrika, Ulaya na Bara ya Asia, pia wanahabari zaidi ya100  watashiriki hii ni fursa kwa Tanzania sio kwa michezo pekee bali ni kukuza Utalii kwani wageni hawa watatembelea hifadhi za taifa na zanzibar" amesema

Amesema katika mkutano wa kesho nchi kadhaa duniani zitafatilia matangazo ya moja kwa moja na baadaye uzinduzi wa mashindano mapya ya Super CUP .

"Timu ambazo zitapata fursa kushiriki mashindano haya makubwa zitajulikana kesho kutokana na viwango vya timu vilivyopangwa na CAF" amesema

Maandalizi ya mkutano huo, yanaendelea katika kituo cha mikutano c ha Arusha, AICC huku pia mikutano ya kamati mbali mbali za CAF ikiendelea katika hoteli kadhaa jijini Arusha.