Shangazi amrithi Barbara

Mbunge wa Jimbo la Mlalo, Rashid Abdallah Shangazi ambaye ni Mwenyekiti wa tawi la Simba Bungeni maarufu ‘Wekundu wa Mjengoni' ameteuliwa kuwa Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba akichukua nafasi ya Barbara Gonzalez, aliyeteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu wa klabu.

Kupitia ukurasa wao wa mitandao ya kijamii wa Simba wameandika Shangazi ni mtu anayeamini katika kufanya kazi kwa umoja na kuongoza umma kwa nguvu ili kuleta mafanikio chanya na haogopi kuchukua hatua yoyote.

Wameongeza kuwa pia ana uwezo wa kufanya kazi kwa kujitegemea katika mazingira ya mabadiliko na changamoto kwenye muda uliowekwa na vipaumbele.

Kuhusu uzoefu wake Simba wamesema ana ujuzi mzuri wa masuala ya Uendeshaji wa Biashara na mwenye shauku ya kusaidia makundi mbalimbali katika jamii ili kufikia malengo yao. "Yeye ni mtu bora anayetamani kutoa ubora katika kila fursa," wameeleza Simba

Barbara aliteuliwa kushika nafasi hiyo Septemba 5, 2020 na kuwa mwanamke wa kwanza nchini kushika nafasi hiyo kubwa kwa ngazi za klabu za Ligi Kuu.