Simba kuongeza mafundi wawili

Muktasari:

  • Mwenyekiti wa kamati ya usajili wa Simba, Kassim Dewji amesema ataongeza wataalam wawili wa usajili kwenye jopo lake tayari kwa usajili wa dirisha dogo la Desemba.

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa kamati ya usajili wa Simba, Kassim Dewji amesema ataongeza wataalam wawili wa usajili kwenye jopo lake tayari kwa usajili wa dirisha dogo la Desemba.

“Kuna maboresho ambayo nataka kuyafanya katika Kamati ya usajili yatakwenda ndani ya Bodi kama yatapata ridhaa ya Bodi

Katika utaratibu wetu wa usajili tuna kanuni na taratibu zetu, mchezaji wa nje awe anacheza timu ya Taifa na pia tuangalie ukanda ambao anatokea mfano sehemu ambayo soka liko juu tunaangalia anacheza timu gani,” alisema.

“Wajumbe wengi waliopo kwenye kamati ya usajili nimeshafanya nao kazi ambao ni Mulamu Ng’hambi, Crescentius Magori Magori na Nassoro tunafahamiana na tumefanya kazi pamoja,” alisema.

Amesisitiza pia kuwa endapo kocha atahitaji mchezaji au wachezaji dirisha dogo watafanya hivyo huku akisisitiza kuwa ukanda wa Afrika mchezaji yeyote watakayemuhitaji atasajiliwa bila kizuizi chochote.

“Timu imefanya vizuri misimu minne mfululizo imeondokewa na wachezaji wawili haiwezi kuyumba matokeo yanayopatikana sasa ni sehemu ya matokeo hatuna hofu yoyote kwanza hatujaanza vibaya kwenye ligi kutolewa kimataifa ni matokeo ambayo yalitushtua,” alisema na kuongeza kuwa;

“Hakuna aliyeyatarajia matokeo hayo kilichotokea kuna shida kubwa ndani ya timu si jambo la kuliweka wazi tunalifanyia kazi na mambo yatakuwa sawa lakini ninachotaka kuwaambia wanachama na mashabiki simba ni bora na ina kikosi bora,” alisema.

Alisema wakitaka mchezaji kutoka Ghana, Nigeria, Sudan, Morocco, Zambia wakihitaji mchezaji yeyote kwa gharama yoyote wanauwezo wa kumnyakua huku akisisitiza kuwa kwa levo waliyoifikia Simba hawana klabu ya kushindania mchezaji.

Dewji nafasi aliyopewa alisema sio mpya kwake aliyawahi kuwa Mwenyekiti kabla hajabadilishwa na kuwa mjumbe chini ya marehemu Zacharia Hans Poppe.

“Tulikuwa tunafanya kazi kwa pamoja vizuri kilichobadilika sasa ni kupanda nafasi tu nina uzoefu mkubwa kwenye sekta hiyo na mwaka huu nataka kufanya mabadiliko.”

“Simba inapesa inaweza kusajili mchezaji yeyote lakini mimi upande wangu ni muumini sana wa kutumia wachezaji wa nyumbani kama nitapata nafasi nitakuwa nawapa nafasi sana nyota wa kitanzania faida yake ni kubwa licha ya kufanikiwa kwenye timu yetu na hata timu ya Taifa,” alisema.