Ubabe Mkwakwani Makomandoo wazichapa

Joto la mchezo wa Coastal Union dhidi ya Yanga joto limezidi kupanda huku presha ikiongezeka baada ya makomandoo wa timu zote mbili kuzichapa kavukavu.

Tukio hilo lilichukua nafasi muda mfupi baada ya timu zote kuingia uwanjani tayari kwa mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mapema Coastal Union ambao ndio wenyeji walitangulia kuingia uwanjani wakitinga Mkwakwani saa 8:12 mchana.

Dakika nane baadaye Yanga wakafuata nyuma wakiingia uwanjani hapo huku ulinzi wa wanachama na mashabiki wao ukiwa mkali kwa timu zote.

Hata hivyo vurugu hizo ziliibuka dakika chache baada ya timu hizo kuingia katika maeneo yao ya kubadilishia nguo ambapo ubishani ukaibuka huku wale wa Coastal walionekana kuwalalamikia wenzao wa Yanga.

Tukio hili lilizidi kushika kasi kwa makomandoo hao kushikana mashati na kupigana kwa sekunde kadhaa.

Hata hivyo askari wa Jeshi la polisi walichukua nafasi na kuwatenganisha mashabiki wote na kila mmoja kuelekea upande wake.

Katika tukio lingine, baadhi ya mashabiki waliopo uwanjani hapo walionekana kumzonga na kumvuta mmoja wa watu aliyekuwa uwanjani hapo amevalia jezi ya Simba ili wachezaji wa Yanga wapite.